TIMU YA WATAALAM WA BENKI YA DUNIA YAPANDA MITI HIFADHI YA TAIFA MIKUMI

 

..................

Na Sixmund Begashe

Timu ya wataam kutoka Benki ya Dunia wanaosimamia Mradi wa Kuboresha Usimamizi wa Maliasili na Kukuza Utalii Kusini mwa Tanzania (REGROW) inayoongozwa na Dkt Enos Esikuri imefanya zoezi la upandaji miti katika Hifadhi ya Taifa Mikumi kama sehemu ya mkakati wa kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi.

Akizungumza baada ya zoezi la upandaji miti katika Hifadhi hiyo, Dkt. Esikuri amesema, wameamua kuweka alama ya kudumu kama sehemu ya kuelimisha umma juu ya umuhimu wa Uhifadhi endelevu wa Ikolojia katika maeneo yaliyohifadhiwa Kisheria.

Dkt. Esikuri ameongeza kuwa, Hifadhi ya Mikumi inamchango mkubwa kwa uchumi wa Tanzania hivyo itakapokuwa na uhai wa Ikolojia endelevu itasaidia uhai wa Wanyamapori ambao ndio kivutio kikubwa cha Watalii wa ndani na nje ya nchi na kuifanya Tanzania iongeze pato la Taifa litakalo saidia kuinua maisha ya Watanzania.

Aidha Dkt. Esikuri na wataalam wengine wa Benki ya Dunia wameendesha zoezi la upandaji miti Hifadhi ya Taifa Mikumi kama sehemu ya maandalizi ya ya Mapokezi ya watalii wengi zaidi watakao miminika baada ya ujenzi wa Kiwanja cha ndege cha Kikoboga ambao kinajengwa kupitia mradi wa Kuboresha Usimamizi wa Maliasili na kuboresha Utalii Kusini mwa Tanzania (REGROW) unaotekelezwa kwa mkopo wa masharti nafu kutoka Benki ya Dunia.

Akizungumza baada ya zoezi la upandaji miti Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Hifadhi ya Taifa Tanzania (TANAPA) Kanda ya Mashariki Massana Mwishawa ameipongeza Benki ya Dunia kwa kuendelea kushirikiana na Wizara ya Maliasili na Utalii katika Uhifadhi endelevu wa Maliasili na Kukuza Utalii Kusini mwa Tanzania na kuahidi kuwa TANAPA itahakikisha miti yote iliyopandwa itatunzwa kikamilifu kama urithi si kwa watanzania tu bali kwa watu wote Duniani hususani kwa watakao tembelea Hifadhi hiyo.

 

0/Post a Comment/Comments