TCB NA METRO LIFE ASSURANCE WAZINDUA BIMA BENKI


Kamishna wa Bima Tanzania Dkt. Baghayo Saqware akiwa pamoja na viongozi wa Benki ya TCB pamoja na Kampuni ya  Metro Life Assuarance mara baada ya kuzindua bidhaa mpya ya Benki Bima kupitia huduma za ADABIMA na Saccos Schemes Credit Life
************
Na Mwandishi wetu

BENKI ya Biashara Tanzania (TCB) kwa kushirikiana na kampuni ya Metro Life Assurance wamezindua Bima Benki yenye lengo la kutoa huduma mbili za Bima ziitwazo ADABIMA na Saccos Schemes Credit Life.

Akizungumza na waandishi wa Habari leo Mei 17,2024 Jijini Dar es Salaam, Kamishna wa Bima Tanzania, Dkt. Baghayo Saqware amesema kiini cha huduma hizo ni kujenga uelewa wa umuhimu wa elimu katika kujenga kesho bora ya jamii.

Dkt. Baghayo akizungumzia kuhusu  ADABIMA,  amesema huduma hiyo ni maalum kwa ajili ya ada ya shule inayokamilisha kiu ya mzazi au mlezi kumwona mtoto wake akifanikiwa kwa kupata elimu bora anayostahili ambapo bidhaa hiyo ilithibitishwa na Mamlaka mnamo tarehe 22 Novemba 2023.

“Kama tujuavyo wote, majanga ni jambo lisiloepukika katika maisha yetu. Si mara zote mipango yetu inatimia kama tunavyokusudia. Majanga hutokea katika nyakati tusizotegemea na kuvuruga mipango yetu na familia zetu.”

“ADABIMA ni suluhisho la changamoto hizi za maisha, lakini pia ni ahadi kwa wateja kwamba lolote litakalotokea kampuni yake itasimama pamoja naye kuhakikisha mtoto anasoma na kuhitimu masomo yake bila kadhia yoyote ile.” Amesema Dkt. Baghayo

Kuhusu Saccoss Schemes Credit Life Insurance, Dkt. Baghayo amesema ni huduma ya bima maalum kwa ajili ya wadau wa SACCOS na Vikundi vya huduma ndogo za fedha (micro-finance).

Amesema Mamlaka itahakikisha huduma hiyo inaendelea kuwapa watumiaji usalama wa kifedha, utulivu, kujiamini na amani.

“Wadau hawa wanajenga kesho iliyo bora kwa kuinua uwezo wa watoa mikopo na kuwahakikishia wakopaji usalama na umiliki wa mali zao endapo watashindwa kulipa.” Ameeleza

Kwa upande wake Mkuu wa Kitengo cha Bima kutoka Benki ya TCB, Francis Kaaya amesema Bima hizo ni kielelezo cha dhamira ya Benki ya TCB ya kuwasikiliza na kuwahudumia wateja kadri ya mahitaji yao na kuwahudumia watanzania kwa ujumla.

“Tunaelewa umuhimu mkubwa wa elimu katika kujenga kesho bora ya jamii yetu. Bima hii inawapa usalama wa kifedha, lakini pia inalea ndoto na matarajio ya wateja wetu.

Ameendelea kufafanua kuwa, “Bima hizi ni kielelezo cha dhamira ya TCB Benki ya kuwasikiliza na kuwahudumia wateja kadiri ya mahitaji yao na kuwahudumia Watanzania wote kwa ujumla.” Alieleza Kaaya.

Kamishna wa Bima Tanzania Dkt. Baghayo Saqware akionganisha baadhi ya maumbo ya maneno kuashiria kuzindua bidhaa mpya ya Benki Bima kupitia huduma za ADABIMA na Saccos Schemes Credit Life.
Kaimu Mtendaji Mkuu wa Benki ya TCB, Jema Msuya akizungumza wakati wa uzinduzi wa bidhaa mpya ya Benki Bima kupitia huduma za ADABIMA na Saccos Schemes Credit Life 

Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Bima ya Metro Life Assurance, Amani Boma akizungumza wakati wa uzinduzi wa bidhaa mpya ya Benki Bima kupitia huduma za ADABIMA na Saccos Schemes Credit Life .




 

0/Post a Comment/Comments