MHE.NDERIANANGA AZINDUA MPANGO NA MKAKATI WA KUPUNGUZA VIATARISHI VYA MAAFA WILAYA YA KIBITI.

Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu),Mhe. Ummy  Nderiananga akizungumza kabla ya Kuzindua Nyaraka za Usimamizi wa Maafa kwa Wilaya ya Kibiti Mkoani Pwani.

Mkuu wa Wilaya ya Kibiti Mhe. Kanali Joseph William Kolombo akizungumza wakati akitoa utambulisho katika Hafla ya Uzinduzi wa Nyaraka za usimamizi wa Maafa kwa Wilaya ya Kibiti Mkoa wa Pwani.
Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu),Mhe. Ummy Nderiananga (katikati) wakati akizindua Nyaraka za Usimamizi wa Maafa kwa Wilaya ya Kibiti Mkoani Pwani.
Mkurugenzi Idara ya Menejimenti ya Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu Brigedia Jenerali Hosea Ndagala akitoa maelezo mafupi kuhusu utekelezaji wa kazi za kutoa mafunzo kwa kamati pamoja na maandalizi ya Nyaraka ya Usimamizi wa Maafa Wilaya ya Kibiti Mkoa wa Pwani.
Mratibu wa Masuala ya Maafa kutoka Shirika la Mpango wa Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) Bw. Abbas Kitogo akitoa salamu kutoka Shirika hilo katika Hafla ya Uzinduzi wa Nyaraka za Usimamizi wa Maafa kwa Wilaya ya Kibiti Mkoani Pwani.
Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu),Mheshimwa Ummy Hamis Nderiananga kwenye picha ya pamoja na wataalam waliotekeleza kazi za kutoa mafunzo kwa kamati pamoja na maandalizi ya Nyaraka ya Usimamizi wa Maafa Wilaya ya Kibiti Mkoa wa Pwani.

(PICHA ZOTE NA OFISI YA WAZIRI MKUU)

.........................

NA: Issah Moahmed –Pwani.

 EMAIL: issahmohamedtz@gmail.com

Naibu waziri, Ofisi ya waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya sera Bunge na uratibu Ummy Nderiananga amesema serikali imekusudia kusimamia na kuratibu shughuli za kuzuia na kukabiliana na majanga yakiwemo yale yanayovuka mipaka ya Nchi.

Ametoa kauli hiyo Wilayani Kibiti Mkoani Pwani wakati akizindua nyaraka za usimamizi wa maafa ambapo amesema usimamizi huo utazingatia sera ya Taifa ya menejimenti ya maafa ya mwaka 2004 na sharia ya usimamizi wa maafa namba 6 ya mwaka 2022.

Amesema kazi ya uandaaji wa mpango wa kujiandaa na kukabiliana na maafa na Mkakati wa Kupunguza Viatarishi vya Maafa kwa Wilaya ya Kibiti ni muendelezo wa utekelezaji wa jukumu hilo la msingi la Ofisi ya Waziri Mkuu ambalo limelenga kuimarisha usimamizi na uratibu wa Maafa katika ngazi za Mikoa na Wilaya.

‘’Lakini niseme tu Ofisi yetu dhamira yake ni kuzifikia wilaya zote kuwa katika mpango huu, kwa kuanzia tumeamua tuanze na wilaya ya Kibiti serikali itaendelea kusimamia shughuli za kuzuia na kukabiliana na maafa yakiwemo yanayovuka mipaka ya Nchi’’ Amesema Nderiananga.

Kwa upande wake Mkurugenzi Idara ya Menejimenti ya Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu Brigedia Jenerali Hosea Ndagala amesema Ofisi kwa kushirikiana na Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa –UNDP, imetoa mafunzo katika wilaya ya Kibiti na Rufiji kwa njia ya nadharia na vitendo.

 

‘’Mkoa wa Pwani ni miongoni mwa mikoa iliyopata mafuriko na kusababisha madhara makubwa katika wilaya za Kibiti, Rufiji na Mafia ambapo tayari serikali ilishafanya tathmini ya madhara kwa wananchi’’ Amebainisha Brigedia Jenerali Ndagala.

 

Naye Mkuu wa wilaya ya Kibiti Kanali Joseph Kolombo amesema mafunzo hayo yatawasaidia katika kukabiliana na maafa mbalimbali ikiwemo Mafuriko.

 

‘’Pamoja na maafa ya mafuriko wilaya ya Kibiti imepitiwa na miradi ya kimkakati ikiwemo bomba la mafuta kwahiyo mafunzo haya yatatusaidia sana kipindi cha mafuriko’’ Amesema Kanali Kolombo

 

Mafunzo hao yamelenga kuimarisha kamati za usimamizi wa maafa kwa kufahamu majukumu yao kisheria, mfumo wa usimamizi wa maafa nchini pamoja na utekelezaji wa shughuli mbalimbali za maafa kwa vipindi tofauti.

0/Post a Comment/Comments