Na Mussa Khalid Dar es salaam
TUME ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU) imewataka
wananchi kuepuka kupotoshwa na watu wanaojiita mawakala au washauri wanaodai
wanatoa huduma ya jinsi ya kujiunga na vyuo vya elimu ya hapa nchini.
Katibu Mtendaji wa TCU Prof.Charles Kihampa ametoa
wito huo leo jijini Dar es salaam wakati akitoa taarifa kuhusu kufunguliwa kwa
dirisha la Udahili kwa waombaji wa Shahada ya kwanza katika Taasisi za elimu ya
juu kwa mwaka wa masomo 2021/2022.
Prof Kihampa amesema kuwa waombaji wanapaswa
kuzingatia masuala muhimu ikiwa ni pamoja na kusoma mwongozo wa udahili
uliotolewa na TCU kwa makini na kuelewa kabla ya kuanza kutuma maombi ya
udahili.
Aidha Katibu huyo Mtendaji ametoa utaratibu
kwa makundi mbalimbali ya uombaji huku akiwataka kujiepushwa kupotoshwa na
washauri au mawakala wanaodai wanatoa huduma ya kujiunga na vyuo vikuu.
‘Waombaji wenye vyeti vilivyotolewa na
mabaraza ya mitihani nje ya nchi ni lazima wawasilishe vyeti vya Baraza la
Mitihani Tanzania (NECTA) kwa vyeti vya Elimu ya Sekondari au Baraza la Taifa
la Elimu ya Ufundi (NACTE) kwa vyeti vya Stashahada ili kupata ithibati ya
ulinganifu wa sifa zao kabla ya kutuma maombi ya udahili’alisema Profesa Kihampa
Profesa Kihampa amewataka pia kuzingatia
kuwasiliana na vyuo moja kwa moja na kupata taarifa za kina kuhusu program za
masomo ili kujiridhisha kabla ya kutuma maombi.
Tume hiyo imesema mategemeo yao kwa wanaoweza
kupata udahili kwa mwaka huu kwenye vyuo yatakuwa zaidi ya laki moja kwani
udahili umeendelea kuongezeka kila mwaka.
Hata hivyo Tume hiyo imetoa wito kwa waombaji
wa udahili na wananchi kuhudhuria Maonyesho ya 16 ya Elimu ya Juu,Sayansi na
Teknolojia yanayotarajiwa kufanyika katika Viwanja vya Mnazi Mmoja jijini Dar
es salaam kuanzia Julai 26 mpaka 31 mwaka huu.

Post a Comment