SERIKALI YA MKOA WA TANGA KUWAUNGA MKONO WANAKIJIJI WA KIJIJI CHA NKELEI.

Mkuu wa Mkoa wa Tanga Adam Malima (picha na mtandao)

Baadhi ya majengo ya Sekondari ambayo yamejengwa kwa umoja wa wanakijiji cha Nkelei

..........................................

NA MUSSA KHALID

Mkuu wa Mkoa wa Tanga Adam Malima amewapongeza wananchi wa Kijiji cha Nkelei kilichopo Kata ya Rangwi Wilaya ya Lushoto kwa kujitolea kuiunga mkono serikali kwa Kujenga Vyumba vya Mdarasa ya Sekondari pamoja na Zahanani ya Kijiji hicho.

Akifanya Mahojiano na mwandishi wa habari hizi Mkuu huyo wa Mkoa amesema kwa kuonyesha ushirikiano kwa wananchi hao amewasisitiza Wakurugenzi katika kupelekea pesa za ndani za maendeleo watoe kipaumbele kwa maeneo ambayo wananchi wamejitolea nguvu zao kwa kujenga miradi ya kimaendeleo.

RC Malima amesema popote wanapohitaji nguvu ya kuwasaidia lazima serikali ya Mkoa iwaunge mkono ili kufanikisha kwa wakati miradi hiyo ya wananchi ili kuweza kurahisisha huduma na waondokane na changamoto ya kwenda umbali mrefu kutafuta huduma.

‘Kwanza wananchi wanaojikusanya wakajenga Sekondari pamoja na Zanahani wanajielewa sana na ndio maana hata mimi katika kuwepo Tanga huwa nawaambia tukitaka kufanya maendeleo kwa wananchi tujikite kuwaangalia wananchi ambao wameonyesha jitihada za maendeleo kwani hata usimamizi watafanya vizuri’amesema RC MALIMA

Aidha Mkuu wa Mkoa Malima amewaomba wananchi kuendelea kutambua na kusimamia vyema miradi hiyo ya kimaendeleo ili kuepukana na watu wasiopenda maendeleo kwa kuingiza tamaa katika miradi hiyo.

Kwa upande wake Diwani wa Kata ya Rangwi Ramadhani Issa Lyimo amesema malengo yao Sekondari hiyo ambayo imejengwa kwan nguvu za wanakijiji ni kuanza kutumia kuanzia mwezi Januari 2022.

Amesema katika Mradi huo Halmashauri waliwasaidia mabati kwa ajili ya kuezeka lakini pia Ushirikiano Mkubwa unatolewa na vijana wa mjini ambao ni wazaliwa wa kijiji hicho ambao wamehakikisha kila hatua inafanikiwa.

‘Kukamilika kwa miradi hii kutasaidia kwa wanafunzi ambao wanakwenda sekondari ya jirani kijiji cha Goka kutawaondolea kutembea umbali mrefu kwenda shule na hivyo kusoma karibu’amesema Diwani Ramadhani

Ikumbukwe Mwenyekiti wa Maendeleo ya Kijiji kutoka katika umoja wa kikundi Cha Nkelei na Mabadiliko ambacho Makao Makuu yake yapo Jijini Dar es salaam Rasuli Chanoga alisema wamepatiwa mabati hayo 132 ambayo yamesaidia kuezeka madarasa mawili ya awali.

Chanoga alisema kwa mchango huo ambao serikali iliwapatia ni msaada mkubwa kwao kwani adhma yao ni kuwasaidia watoto wapate elimu bora lakini pia kuwaondolea adha na changamoto ya kwenda umbali mrefu kuitafuta elimu.

Aidha Chanoga alisema baada ya kupatiwa mabati hayo matarajio yao mpaka kufika mwezi Januari mwakani madarasa hayo yawe yamekamilika na hivyo wanafunzi kuanza kuyatumia kwa kujifunzia.

0/Post a Comment/Comments