
TAARIFA KWA UMMA
MAADHIMISHO YA SIKU YA MOYO DUNIANI TAREHE 29/09/2021
Katika kuadhimisha Siku ya Moyo Duniani tarehe 29/09/2021 Taasisi ya
Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kushirikiana na Wilaya ya Kigamboni
tutafanya upimaji wa magonjwa ya Moyo bila malipo kwa wananchi wa
Mkoa wa Dar es Salaam na mikoa jirani. Upimaji huo utafanyika katika viwanja
vya Hospitali ya Wilaya ya Kigamboni iliyopo eneo la Gezaulole kuanzia saa
mbili (2) kamili asubuhi.
Upimaji utafanyika kwa watoto
na watu wazima. Wananchi watapimwa urefu, uzito, shinikizo la damu (BP),
kiwango cha sukari mwilini, vipimo vya kuangalia jinsi mfumo wa umeme wa
moyo unavyofanya kazi (Electrocardiogram- ECG) na moyo unavyofanya kazi
(Echocardiogram – ECHO) na kutoa ushauri.
Tutakuwa na wataalamu wa lishe ambao watatoa elimu ya lishe bora ambayo
itawapa wananchi uelewa na kufuata mtindo bora wa maisha ambao
utawasaidia kuepukana na magonjwa ya moyo ambayo ni moja ya magonjwa
yasiyoambukiza na mtu anaweza kuyaepuka kwa kufuata ushauri wa kitaalamu.
Kwa wale watakaokutwa na matatizo ya moyo watafanyiwa uchunguzi zaidi na
kupatiwa matibabu ikiwa ni pamoja na kupewa rufaa ya kwenda kutibiwa katika
Taasisi yetu. Kauli mbiu ya mwaka huu ni: “Tunza afya ya moyo wako ili
utunze maisha ya wengine”.
Tunawaomba wananchi mtumie siku hii kujitokeza kwa wingi kupima afya
zenu hii itawasaidia kujua kama mna matatizo ya moyo au la na hivyo kuanza
matibabu mapema kwani asilimia kubwa ya wagonjwa tunaowapokea katika Taasisi
yetu mioyo yao huwa haiko katika hali nzuri.
Aidha kama mnavyofahamu wizara ya Afya kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais
TAMISEMI hivi karibuni ilizindua mpango wa jamii shirikishi na harakishi wa
uelimishaji dhidi ya chanjo ya ugonjwa wa UVIKO – 19 ambao unalenga kuwafikia
wananchi walioko mbali na vituo vya afya ili wapate chanjo hiyo popote pale
walipo. Tunawaomba wananchi kwa wale ambao bado hawajachanja
kuitumia nafasi hiyo kwenda kupata chanjo hii muhimu ili kujikinga
na kuwakinga wengine dhidi ya UVIKO-19.
Imetolewa na :
Anna Nkinda
Mkuu wa Kitengo cha
Uhusiano na Mawasiliano
Taasisi ya Moyo
Jakaya Kikwete
28/09/2021
Post a Comment