THRDC YATOA MAPENDEKEZO YA KUBORESHA HALI YA DEMOKRASIA NA UTAWALA BORA NCHINI.


Mratibu wa Kitaifa wa Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania (THRDC) Onesmo OLengurumwa (katikati) Afisa Uchachamuzi kutoka THRDC Nuru Maro (kulia) na Mkuu wa Program THRDC Leopold Mosha (kushoto) wakizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es salaam

............................................................

NA MUSSA KHALID DAR ES SALAAM

Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania (THRDC) umeitaka serikali kuweka mifumo bora itakayowezesha ushiriki wa watetezi wa Haki za Binadamu na wananchi wote kuweza kushiriki katika chaguzi na Michakato mingine ya Kidemokrasia.

Kauli hilo imetolewa leo jijini Dar es salaam na  Mratibu wa Kitaifa wa THRDC Onesmo OLengurumwa ikiwa ni katika kuadhimisha siku ya Kimataifa ya Demokrasia duniani ambayo huadhimishwa kila ifikapo septemba 15 ya Kila mwaka.

Mratibu huyo amesema kuwa kwa mujibu wa Mkataba wa Afrika kuhusu Demokrasia katika Ibara ya 4 unazitaka nchi wanachama za umoja wa Afrika kuhakikisha kuwa zinakuza Demokrasia,Misingi ya Utawala wa Sheria na haki za binadamu.

‘Katika kuadhimisha siku hii tunatambua umuhimu wa Demokrasia,Utawala bora na kuheshimu haki za binadamu katika nyanja mbalimbali ili kuhakikisha kuwa maendeleo ya taifa na watu wake yanapatikana’amesema Olengurumwa

Aidha Mratibu huyo wa THRDC amesema Tanzania ikiwa ni moja ya nchi mwanachama wa Umoja wa Mataifa na Umoja wa Afrika,Inayo wajibu wa kuhakikisha kuwa haki za kidemokrasia na utawala bora zinazingatiwa.

‘Uwepo wa Sheria zinazominya uhuru wa kujieleza,kupata taarifa na uhueu wa kujumuika zimeendelea kuwa mwiba mkubwa unaokandamiza uwezekano wa kufurahia demokrasia’amesema Olengurumwa

Akitoa mapendekezo katika kuboresha hali ya demokrasia na utawala bora nchini, Mkuu wa Program THRDC Leopold Mosha amesema serikali isimamie misingi ya Kidemokrasia na Haki za Binadamu kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,Mikataba ya Kikanda na Kimataifa.

Amesema ni vyema serikali ikakubali kutia saini Mikataba mbalimbali ya Kimataifa na Kikanda kuhusu demokrasia,Ikiwemo Mkataba wa Umoja wa Afrika kuhusu Demokrasia,Uchaguzi na Utawala wa mwaka 2007.

Naye Afisa Uchachamuzi kutoka THRDC Nuru Maro ameiomba serikali kujenga dhana ya kushauriana na kujadiliana na Makundi mbalimbali ikiwa ni pamoja na makundi ya kidini,Assasi za Kiraia,Sekta binafsi na wananchi kwa ujumla.

Hata hivyo amependekeza kuwa serikali ifikirie upya uamuzi wake wa kuzuia wananchi na Mashirika yasiyo ya kiserikali kufungua kesi katika Mahakama ya Afrika ya haki za Binadamu na watu.

Siku ya Demokrasia ilianzishwa mwaka 2007 na Mkutano mkuu wa Umoja wa Mataifa ili kuyakumbusha mataifa yote umuhimu wa kusimamia mifumo na misingi duniania ambapo kwa mwaka huu dhima kuu ni’Kuimarisha uthabiti wa Kidemokrasia pindi changamoto zinapojitokeza’

0/Post a Comment/Comments