(Habari na Picha na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Rukwa)
……………………………………………………
Mkoa wa Rukwa licha ya kuwa ni mzalishaji mkubwa wa
mazao ya chakula bado unakabiliwa na tatizo la udumavu unaotokana na lishe duni
hivyo serikali na wadau wamebuni miradi ya lishe bora kupitia kilimo na
ufugaji.
Hayo yamebainishwa na Mratibu wa mradi wa Lishe
Endelevu chini ya Shirika la Save The Children Rukwa Emanuel Magoyo wakati wa
ziara ya wajumbe wa Kamati ya Lishe ya Mkoa iliyotembelea mashamba darasa,
ufugaji kuku, sungura na samaki kwenye wilaya za Sumbawanga na Nkasi mwishoni
mwa wiki hii.
Magoyo alisema mradi umefanikiwa kufundisha vijana
zaidi ya 700 na maafisa ugani 187 toka wilaya za Sumbawanga, Nkasi na Kalambo
kutekeleza miradi ya lishe bora hatua inayosaidia kuondoa tatizo la udumavu
linaloathiri zaidi watoto wadogo.
“Mradi umefankiwa kutoa mafunzo juu ya lishe bora,
teknolojia ya umwagiliaji, kutoa mbegu bora za mazao ya mboga mboga, matunda na
vifaranga vya kuku bora na samaki ili vijana na akina mama wanzishe miradi ya
lishe bora “alisema Magoyo.
Kamati pia ilitembelea shamba darasa la kijana
Morgan Yiskaka wa kijiji cha Milundikwa wilaya ya Nkasi ambaye amefanikiwa
kuzalisha aina 12 za mazao ya mboga mboga na ufugaji samaki ikiwa ni mkakati wa
kuboresha lishe endelevu kwenye jamii.
Akizungumzia mafanikio aliyoyapata chini ya mradi wa
lishe endelevu Yiskaka alisema tangu mwaka 2017 vijana na akina mama wengi
wamepata mafunzo ya kilimo bora toka shambani hapo chini ya uratibu wa Save The
Children.
“Hapa ninazalisha mazao zaidi ya 12 mchanganyiko ili
kuchochea upatikanaji wa lishe bora katika jamii. Sasa nina soko kubwa la mazao
ya mboga mboga kutokana na watu wengi kutambua faida zake kwa afya” alisema
kijana Yiskaka.
Naye Mratibu wa Lishe Mkoa wa Rukwa Teddy Swallo
alisema tafiti za mwaka 2018 za Wizara ya Afya zinaonesha tatizo la udumavu
liko takribani asilimia 47 kwa mkoa wa Rukwa hivyo kuhitaji mikakati ya
kuliondoa kupitia miradi ya lishe endelevu ikiwemo kilimo cha mboga mboga na
ufugaji” alisema Swallo.
Swallo alibainisha kuwa mradi wa lishe endelevu
kwenye mkoa wa Rukwa unalenga kuboresha hali ya lishe kwa akina mama
wajawazito, watoto wadogo na vijana ili waweze kubadili tabia za ulaji chakula
bora.
“Pamoja na kuwa na elimu ya ufugaji au kilimo cha
mboga mboga ni budi tukabadili tabia zetu za kula ikiwemo kupata mlo kamili kwa
makundi yote matano ya nafaka, wanyama, mboga mboga, matunda na mafuta”
alisisitiza Swallo.
Mratibu huyo alitaja madhara ya udumavu kwa watoto
kuwa ni pamoja na kuwa na uwezo mdogo wa kufikiri (akili) na kuwa na uwezekano
mkubwa wa kupata maradhi mbalimbali.
Akizungumzia juu ya mradi wa ufugaji kuku bora
Mkulima Kiongozi wa kijiji cha Mkangale Namanyele Elizabeth Ngalawa alisema
wanashauri wakulima wasipige mahindi dawa zisizo na ubora ili kutoathiri
chakula cha binadamu na mifugo.
Aliongeza kusema kikundi chao kinajihusisha na
ufugaji bora wa kuku aina na Saso pamoja na shamba kilimo ili kujenga tabia ya
kula lishe bora ikiwemo kukuza kipato cha kaya baada ya kupata mafunzo toka
wataalam wa mradi wa USAID/Lishe Endelevu.
Mwisho.
Imeandaliwa na;
Afisa Habari Mkuu,
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Rukwa
SUMBAWANGA
05.09.2021




Post a Comment