MHANDISI KASEKENYA AIPONGEZA TMA KWA KUTOA TAARIFA ZINAZOSAIDIA SEKTA MBALIMBALI.

Naibu Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi Mhandisi Godfrey Kasekenya (mwenye suti nyeusi) alipotembelea banda la Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) na akielezewa kuhusu utendaji wa mamlaka hiyo  leo katika Mkutano wa 14 wa sekta ya Uchukuzi.

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) Dkt Agness Kijazi akizungumza na waandishi wa habari kueleza utendaji kazi wa Mamlaka hiyo.


..........................................

NA MUSSA KHALID,DAR ES SALAAM

Naibu Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi Mhandisi Godfrey Kasekenya ameipongeza Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) kwa kuendelea kutoa taarifa za Hali ya Hewa ambazo zinasaidia katika sekta mbalimbali nchini ikiwemo ya usafirishaji wa ardhini na majini pamoja na uboreshaji wa miundombinu ya kimaendeleo.

Mhandisi Kasekenya ameeleza hayo leo jijini Dar es salaam wakati akizungumza kwenye Mkutano wa 14 wa sekta ya Uchukuzi wenye lengo la kupima utendaji wa sekta mbalimbali za uchukuzi.

Naibu Waziri Mhandisi Kasekenya amesema Taasisi hiyo ni muhimu kwani inasaidia sekta zote katika utekelezaji wa miradi ya kimkakati hususani ya barabara kufahamu taarifa za hali ya hewa kwa yanayotarajiwa kutokea na kwa wakati gani.

Aidha Mhandisi Kasekenya amesema ni vyema katika ujenzi wa miradi yeyote kuhakikisha unafatwa utaratibu wa kitaalamu wa kufahamu mazingira hayo ili kuweza kuepukana na madhara yanayoweza kujitokeza.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) Dkt Agness Kijazi amesema Mamlaka hiyo imekuwa ikitumika kwenye miradi mbalimbali ya maendeleo kwenye sekta ya uchukuzi ikiwemo Anga,kwenye Reli,masuala ya barabara,na miradi mikubwa ya ujenzi hata bwawa la Nyerere ambalo linaendelea na ujenzi.

‘Sisi tupo hapa kuwaonyesha ni huduma gani tunazozitoa na kuwaonyesha jinsi tunatoa utabiri na namna unavyotumika kwani ni muhimu katika sekta hizo na hasa katika kipindi hiki ambacho kuna mabadiliko ya tabia ya nchi DUNIANI hivyo tunawaeleza wanavyoweza kuzitumia tabiri tunazozitoa katika shughuli zao’amesema Dkt Kijazi

Hata hivyo Dkt Kijazi ameziasa taasisi mbalimbali kuangalia masuala ya hali ya hewa ili kuepukana na kuweka mradi mikubwa kisha  baadae likaja janga moja kubwa na kuufuta na kujikuta unanza upya.

Mkutao huo 14 wa sekta ya Uchukuzi umezishirikisha taasisi mbalimbali za kiserikali zikiwemo za usafirishaji wa Ardhini na Majini kwa malengo ya kujadili utendaji kazi wa taasisi hizo katika ufanyaji wa shughuli zao.

0/Post a Comment/Comments