Mwenyekiti wa Kikosi Kazi cha Sensa Kitaifa TASAC Kapt. Alex Katama
Mmiliki
wa chombo cha Uvuvi katika Kisiwa cha Kimoyomoyo kilichopo Wilaya ya Muleba Philemoni
Jacob
Afisa Mfawidhi TASAC mkoa wa Kagera Kapt. David Chiragi
......................................
Na mwandishi wetu.
Serikali
imewataka wananchi kushiriki katika Sensa ya Vyombo Vidogo Majini inayoendelea
kufanyika nchini ili iweze kupata takwimu rasmi zinazohusu vyombo Vidogo vya
Uvuvi na Usafirishaji Majini.
Akizungumza
na Waandishi wa Habari wakati akitoa tathimini ya zoezi hilo, Mwenyekiti wa
Kikosi Kazi cha Sensa Kitaifa, Kapt. Alex Katama amesema zoezi la Sensa linaendelea
vizuri ambapo hadi sasa wamesha hesabu takribani vyombo vidogo vya Uvuvi na
Usafirishaji vipatavyo elf thelathini kwa Tanzania Bara.
“Tupo
katika zoezi la Sensa ya Vyombo vyote vidogo ambavyo vinafanya shughuli ya
Uvuvi na Usafirishaji Majini. Tunapata ushirikiano mzuri sana kutoka kwa viongozi
na wananchi wa maeneo husika na hivyo hata katika maeneo ambayo bado
hatujayafikia, tunaomba wananchi watoe ushirikiano” alisema Kapteni.Katama.
Katama
alisema lengo kuu la Sensa ambayo imeanza kufanyika kuanzia tarehe 01 Oktoba,
2021 na itakamilika tarehe 30 Oktoba, 2021 ni kupata takwimu rasmi za vyombo
vidogo vya Uvuvi na Usafirishaji ili Serikali iweze kujua vipo vingapi,
vinapatikana maeneo gani na vipo katika hali gani.
Alisema
takwimu hizo zitasaidia kupanga mipango mbalimbali ya kuboresha hali ya uvuvi
na huduma ya usafirishaji hasa kwa kutumia vyombo vidogo.
Aidha,
alisema kupatikana kwa takwimu za vyombo hivyo kutasaidia kwenye uwekezaji wa
viwanda vya kusindika samaki na mitambo ya kukaushia dagaa.
Ameongeza
kuwa, Sensa hii itasaidia wavuvi na wasafirishaji kupata taarifa za hali ya
hewa ambazo ni muhimu katika usalama wao.
Akitoa
taarifa ya utekelezaji wa Sensa katika mkoa wa Kagera, Afisa Mfawidhi wa TASAC Kapteni
David Chiragi amesema mkoa wa Kagera ni miongoni mwa mikoa yenye vyombo vingi
vidogo vya Uvuvi na Usafirishaji na hivyo wanatarajia kusajili vyombo vingi
zaidi ukilinganisha na maeneo mengine.
“Serikali
inafanya Sensa ya Vyombo vidogo vya usafirishaji na Uvuvi majini kwa lengo la
kupata takwimu ya idadi na taarifa zingine ambazo zitasaidia kwenye uratibu na
usimamizi wa sekta ya uvuvi na usafirishaji majini” amesema Chiragi.
Amesema
kwa upande wa TASAC, takwimu hizi zitasaidia katika udhibiti maana wataweza
kujua vyombo vipo vingapi, vipo maeneo gani, na katika hali gani na vinafanya
shughuli gani.
Amesema
kujulikana kwa vyombo hivyo kutasaidia katika usalama wa watumiaji wa vyombo
hivyo na usalama wa vyombo vyenyewe.
Chiragi
amesema taarifa wanazokusanya kwenye Sensa hii ni idadi ya vyombo, usajili,
mawasiliano na taarifa za makazi ya mmiliki.
Kwa
upande wake Mwenyekiti wa Kijiji cha Iramba Novatus Bernado amesema wamelipokea
vizuri zoezi la Sensa na wananchi wa eneo lake wametoa ushirikiano vizuri
kukamilisha zoezi hili muhimu la kitaifa.
Alisema
kufanyika kwa Sensa hiyo kutawezesha kuimarisha sekta ya uvuvi na usafirishaji
na katika masuala ya usalama pale inapotokea upotevu wa chombo kinaweza
kupatikana kwa urahisi.
Ametoa
wito kwa wananchi wa eneo lake kujitokeza kwa wingi kuhakikisha vyombo vyao
vinahesabiwa katika Sensa hii ili Serikali iweze kupanga mipango mizuri ya
kuboresha uvuvi na usafirishaji kwa kutumia vyombo vidogo.
Kwa
upande wake Philemoni Jacob Mmiliki wa chombo cha Uvuvi katika Kisiwa cha
Kimoyomoyo kilichopo Wilaya ya Muleba alisema Sensa hii ni nzuri kwani
itawasaidia kutambulika na Serikali na hata ikitokea wamepoteza mitumbwi yao
itakuwa rahisi kuipata kutokana na utambuzi wake kuwa umesajiliwa wapi na nani
anaumiliki.
Aidha,
elimu ya usalama wa usafiri wa vyombo vya majini ilitolewa kwa kuhimiza wavuvi,
waendesha vyombo vya majini kuzingatia kutumia jaketi okozi kwa ajili ya
usalama wao.Elimu hiyo ilitolewa katika mwalo wa Kimoyomoyo, Mrumo, Rulanda,
Katunguru na maeneo mengine.
Sensa ya Vyombo Vidogo vya Uvuvi na Usafirishaji ni Sensa ya kwanza kufanyika nchini kupitia Shirika la Wakala wa Meli Tanzanzania (TASAC) kwa kushirikiana na Wizara ya Mifugo na Uvuvi na Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS).
Post a Comment