WAMACHINGA DAR WAENDELEA KUOMBA KUBORESHEWA MAZINGIRA YA BIASHARA.

Mwenyekiti wa Machinga Mkoa wa Dar es salaam na Makamu Mwenyekiti wa Machinga Kariakoo Namoto Yusuph akizungumza na waandishi wa habari (picha na Mussa Khalid)


...................................

NA MUSSA KHALID

Wafanyabiashara wadogo maarufu kama machinga jijini Dar es salaam wameendelea kuiomba serikali kuboresha mazingira wezeshi ya sehemu wanazopangiwa kufanya biashara zao ili waweze kuepukana na changamoto ya kuwapata wateja.

Wakizungumza na Mwandishi wa habari hizi kwa nyakati tofauti jijini Dar es salaam kuhusu utekelezaji wa zoezi linaloendelea la kutakiwa kuhama na kwenda maeneo waliyopangiwa baadhi ya wafanyabiashara hao wamesema zoezi hilo linawaletea changamoto kwa kutofahamu sehemu wanayotakiwa kwenda.

Mfanyabiashara wa Kariakoo Ramadhani Mkata pamoja na Mama Angel wamesema ni vyema serikali ikaendelea kuchukua jukumu la kuwapanga vyema katika maeneo waliyoyatenga ambayo yatakuwa na changamoto ya ufanyaji wa biashara .

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Machinga Mkoa wa Dar es salaam na Makamu Mwenyekiti wa Machinga Kariakoo Namoto Yusuph amesema zoezi hilo la wamachingwa kuondoka na kwenda walipopangwa limefanyika kwa zaidi ya asilimia 85 kwenye baadhi ya maeneo lakini kumekuwepo na changamoto ya maeneo wanayokwenda.

‘Kwa kusema ukweli mimi ni kiongozi ninawajibu wa kuwakilisha wengi wamachinga wametii maeneo mengi ila changamoto kwenye maeneo ambayo wajasiriamali wanapelekwa kutokuwa rafiki kwa ajili ya ufanyaji wa biashara’amesema Namoto

Naye Mkurugenzi wa Habari na Mawasiliano wa Jumuiya ya Wafanyabiashara Tanzania Stephen Chamle baadhi ya maeneo ya  soko la Kariakoo kumekuwa na changamoto kutokubaliana na utaratibu hivyo ameiomba serikali ya mkoa kutumia hekima kuwapeleka sehemu zitakazowasaidia kufanikiwa na ufanyaji wa shughuli zao pasipo bugudha yeyote.

‘Sisi kama Jumuiya ya Wafanyabiashara Tanzania agizo la Mhe Rais tumelipokea hivyo tunadhani ni wajibu wa mamlaka za chini kufanya utekelezaji wa jambo hili kuwa utulivu mkubwa nikizungumzia eneo la kariakoo bado kunachangamoto ya baadhi ya maeneo wameweza kuondoka kwa hiari lakini wengine bado wapo na ubishani usio na afya kwa taifa kwa kutaka kuhalalisha maeneo ya barabara kufanyia biashara ’amesema Chamle

Ikumbukwe kuwa hivi karibuni Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam alitoa onyo kwa wafanyabiashara wanaoendelea kufanya biashara pembezoni mwa barabara licha ya vibanda vyao kuondolewa,amewataka kuhama na kwenda kwenye maeneo yaliyotengwa.

0/Post a Comment/Comments