WIZARA YA ELIMU YAWAPATIA VITABU NA VIFAA WANAFUNZI WASIOONA NA WENYE UWONI HAFIFU TANZANIA BARA NA ZANZIBAR

..................

NA SALYM BITCHUKA

Serikali kupitia  Wizara  ya  Elimu , Sayansi na Teknolojia imeahidi  kuendeleza  kazi  nzuri ambayo  Rais Samia Suluhu Hassan ameelekeza  ya  kuhakikisha wanafunzi  wenye  mahitaji  maalum  wanapewa  fursa sawa  kwa  kuwapatia  mahitaji  wezeshi ikiwemo  vitabu  na vifaa maalum na saidizi  vitakavyowawezesha  kujifunza  sawasawa na wanafunzi  wengine kwa  lengo  la kuboresha  ujifunzaji wao.

Kauli  hiyo  imetolewa  leo  jijini  Dar  es Salaam na  Waziri wa Elimu , Sayani na Teknolojia Profesa  Adolf  Mkenda wakati  wa  Uzinduzi wa  kazi ya ugawaji wa vifaa  na  vitabu kwa  kidato  cha kwanza  mpaka cha  sita vya Breli na maandishi yaliyokuzwa  pamoja na ugawaji wa vifaa kwa wanafunzi wenye mahitaji maalum  wa vyuo vikuu .

Akizungumza  katika  Uzinduzi  huo Profesa  Mkenda amesema  vitabu  hivyo vinakusudiwa kusambazwa  kwa wanafunzi  3,677 katika  shule 764  za  wanafunzi  wasioona  na wenye  uwoni  hafifu  Tanzania  Bara na  Zanzibar.

Aidha  Profesa  Mkenda  amesema  mbali  na vitabu  hivyo serikali kupitia  mpango  huo wa  maendeleo  wa  ustawi  wa taifa  na mapambano  dhidi ya  uviko – 19  imefanikisha  kutoa kiasi  cha  shilingi milioni  770 kwa ajili  ya  kununua vifaa maalum  na saidizi 413 kwa  ajili  ya wanafunzi  wenye  mahitaji  maalum  waliopo kwenye  vyuo  vikuu  kumi  na  moja  nchini

Kwa  upande  wake  Mkurugenzi  mkuu  wa  Taasisi  ya  Elimu  Tanzania (TET ) Anneth  Komba  amesema  vitabu vya  Braili vimechapishwa  nchini  kupitia  kiwanda  pekee  kilichopo  hapa  nchini chenye  uwezo  wa  kuchapa vitabu  vyenye maandishi ya Braili  na mpaka  sasa  kupitia   kiwanda  hicho  TET  imesha  chapa vitabu vyote vya Kiada  vya  elimu  ya   msingi pamoja  na nyaraka  za mitaala, huku  mkurugenzi  wa Elimu Maalum  kutoka  wizara ya elimu  Sayansi  na Teknolojia Dkt .Magreth Mathonya  akiwataka wazazi  wenye  watoto  wenye  uhitaji  maalum  kuwapeleka  shuleni  badala  ya kuwaacha  nyumbani

Sanjari  na  hayo  Serikali  kupitia  wizara  ya   Elimu  Sayansi  na  Teknolojia  imeshauriwa kufanya sensa ya vijana na watoto wenye mahitaji maalum pamoja  na kukagua miundombinu yao ili kufanikisha upatikanaji wa elimu  sawa na sahihi  kwa kila mtoto wa Kitanzania . 

0/Post a Comment/Comments