BARUA YA BABA YOHANE PAULO II HAIONEKANI KATIKA MAISHA HALISI YA SASA

Picha ya Pamoja ya Viongozi wa Pro-life Tanzania na Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam, Mhashamu Henry Mchamungu. ( Maktaba)

.....................

NA Frida Manga

Imeelezwa kwamba Barua ya Kichungaji ya Baba Mtakatifu Yohane Paulo II (Familiaris Consortio 1981) kuhusu Nafasi ya Familia Katika Ulimwengu wa leo haionekani katika maisha halisi ya sasa.

Na hii ni kutokana na ukuaji wa Utandawazi na Maisha ya Kisasa yanayotajwa kuharibu familia.

Hayo yameelezwa  katika Mkutano wa  Shirika la Kutetea Uhai Tanzania ( Pro-Life Tanzania) uliojadili barua hiyo ya Kichungaji na kugundua kuwa haiakisi maisha halisi ya mwanadamu wa sasa au familia.

Mkutano huo uliokuwa ukijadili Insikliko ya Baba Mtakatifu ulishirikisha Watetezi wa Uhai kutoka nchi za Tanzania, Kenya, Uganda Zambia, Zimbabwe na Rwanda.

Na kwa upande wake Katibu wa Pro-life Tanzania Godfrey Rahabu Mkaikuta alisema maisha yamebadilika kulingana na ukuaji wa Teknolojia na kwamba hali hiyo imepelekea Vijana kujiongoza ama kujilea wenyewe bila Wazazi au Walezi.

" Familia kukaa pamoja katika mlo, Sala na mazungumzo ni ishara ya Upendo na heshima lakini katika maisha ya sasa, jambo hilo halipo Kabisa, Wazazi ama Walezi wako bize  na majukumu kiasi cha kuwaacha Watoto peke yao" alisema Mkaikuta.

Kwa mujibu wa Mkaikuta Barua ya Kichungaji ya Baba Mtakatifu inatamka juu ya Malezi bora kwa Watoto na Vijana yanayozingatia Uchaji wa Kimungu, Ushirikiano na kuheshimu Utu wa mwanadamu.

Watoto wanajiongoza wenyewe na katika makuzi yao wanakutana na changamoto nyingi, na kujikuta wakiiga na kufuata mambo yanayokwenda kinyume na tamaduni Mila na Imani.

Kutokana na hivyo Pro-life imekusudia  kupeleka ujumbe wa barua hiyo ya Kichungaji kwa vijana katika ngazi ya Vyuo Vikuu.

Alisema mpango huo unakusudiwa kuanza kutekelezwa mapema Januari mwakani katika Vyuo vya Kati, Vidogo na Vyuo Vikuu vya Kanisa Katoliki na tayari wameshajipanga katika makundi namna ya kufikia Vijana hao katika Vyuo.

0/Post a Comment/Comments