Mkuu wa mkoa wa Dodoma Rosemary Senyamule amekabidhi rasmi kwa mkandarasi utekelezaji wa mradi wa bwawa la Umwagiliaji Msagali Chunyu wilayani Mpwapwa Mkoani Dodoma litakalogharimu Tsh.Bilioni 27 zilizotolewa na Rais Samia Suluhu Hassan huku akitoa maagizo utekelezaji wa mradi huo uanze kwa wakati ili kuleta manufaa kwa wananchi.
Akizungumza katika eneo hilo la utekelezaji wa mradi, mkuu huyo wa mkoa amesema ni muhimu mkandarasi anayetekeleza mradi huo kuanza kutekeleza mradi huo kwa wakati kwani dhamira ya Rais Samia ni kuleta mapinduzi katika sekta ya kilimo.
Mkuu wa Wilaya ya Mpwapwa Mwalimu Josephat Maganga amekataza uuzaji ovyo wa ardhi katika eneo hilo ili kuepusha migogoro hapo baadae.
Nao watekelezaji wa mradi huo akiwemo mhandisi mkoa wa Dodoma Raphael Raizer pamoja na mhandisi wa mradi huo Emmanuel Mponda wamezungumzia namna mradi huo utakavyotekelezwa.
Mradi wa bwawa hilo utachochea ukuaji wa uchumi kupitia sekta ya kilimo kwa wananchi wilaya ya Mpwapwa ambapo unatarajiwa kuanza Oktoba 2022 na kukamilishwa Machi,2024 na litakuwa na uwezo wa kuzalisha lita za maji trilioni 90.



Post a Comment