Kamanda wa Polisi mkoa wa Kagera,William Mwampaghale,akiwaonyesha waandishi wa habari silaha na risasi zilizopatikana kwenye tukio la uhalifu.
Kamanda wa polisi mkoani Kagera, William Mwampaghale,akiwaonyesha waandishi wa habari aina ya mabomu yaliyokamatwa kwenye tukio la uhalifu wilayani ngara.
WATU wawili wanaodhaniwa majambazi wameuawa kwa kupigwa risasi na polisi wilayani ngara mkoani kagera kisha kukamata silaha ya kivita aina ya AK 47,risasi 25 pamoja na mabomu mawili ya kutupa kwa mkono.
Marehemu hao ambao hata hivyo hawajafahamika majina yao na wanakadiliwa kuwa na umri wa kati ya miaka 25 na 30, miili yao imehifadhiwa kwenye chumba cha kuhifadhi maiti kwenye hospitali ya Nyamiaga kwaajili ya utambuzi na uchunguzi zaidi.
Hata hivyo imedaiwa kwa watu hao walipanga kufanya uharifu wa kutumia silaha kwenye kijiji cha Kumunazi kwa lengo la kujipatia mali kwa njia isiyo halali huku pongezi nyingi zikielekezwa kwa jeshi la polisi kufanikiwa kudhibiti tukio hilo kabla halijasababisha madhara kwa wananchi.
Kamanda wa polisi mkoa wa Kagera,William Mwampaghale, ameviambia vyombo vya habari kuwa tukio hilo limetokea kwenye kijiji cha Kumunazi barabara ya kuelekea Rulenge wilayani Ngara na kwamba jeshi hilo lilipokea taarifa za maandalizi ya uhalifu huo kutoka kwa wananchi wasamaria wema.
"Baada ya taarifa hizo tuliweka mitego kwenye barabara zote zinazoingia Kumunazi na ilipofika majira ya saa 3:35 usiku ilipita pikipiki iliyokuwa imebeba watu watatu...baada ya askari wetu kuwasimamisha walikaidi wakalazimika kupiga risasi hewani ili kuwafanya wajisalimishe lakini waliendelea kupuuza" amesema.
" Ndipo askari wakalazimika kuishambulia pikipiki hiyo kwenye mataili ili iishiwe upepo kwa lengo la kuwakamata watuhumiwa hao...lakini kwa bahati mbaya baadhi ya risasi ziliwapata wawili waliokuwa wamebebwa na kwamba mtu mmoja alipigwa kwenye paja la kushoto na mwingine kwenye kiuno huku dreva wa pikipiki hiyo akifanikiwa kutokomea polini"amesema Kamanda Mwampaghale.
Amedai kuwa wakati askari wakifanya upekuzi kwenye makoti waliyokuwa wamevaa watu hao,walifanikiwa kukamata silaha moja aina ya AK 47,risasi 25, pamoja na mabomu mawili ya kutupa kwa mkono na kwamba jitihada za kutaka kunusuru maisha yao ziligonga mwamba baada ya kufariki wakati wakiwahishwa hospitali.
Kamanda Mwampaghale, ametumia fursa hiyo kuwaonya watu wote wenye nia ya kufanya uharifu kwenye mkoa wa Kagera kwa madai kuwa doria za magari,pikipiki na miguu zimeimalishwa kwa kushirikiana na polisi wa mikoa jirani ya Geita na Kigoma.
Aniceth Lweyongeza, mkazi wa Ngara mjini amelishukuru jeshi la polisi kwa kudhibiti matukio ya uharifu kabla ya kutekelezwa na kwamba inawafanya waishi kwa amani na kuongeza mwitikio wa uzalishaji mali ili kuinua uchumi wao.
Mwisho.




Post a Comment