Mamlaka
ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA) imeendelea na operesheni ya
kukamata, kuharibu na kuteketeza dawa za
kulevya aina ya bangi katika wilaya ya ARUMERU mkoani Arusha na kufanikiwa
kukamata jumla ya gunia 731 za bangi kavu pamoja na kuteketeza hekari 308 za
mashamba ya bangi.
Operesheni
iliyofanyika 01 June, 2023, katika kijiji cha Lesinoni, jumla ya gunia 249 za bangi kavu zilikamatwa huku hekari 207
za mashamba ya bangi ziliteketezwa huku operesheni iliyofanyika tarehe 31 Mei
2023, katika kijiji cha Kisimiri juu,
Mamlaka ilikamata gunia 482 za bangi na kuteketeza jumla ya hekari 101 za
mashamba ya bangi. Watuhumiwa 9 wamekamatwa kuhusiana na matukio hayo.
Kwa
mujibu wa taarifa kwa Umma iliyotelewa na Kamishna Jenerali Aretas Lyimo leo imesema
kuwa operesheni hiyo imefanyika kufuatia agizo la Rais wa Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan la kufanya operesheni nchi nzima ili
kuhakikisha dawa za kulevya zinatokomezwa nchini.
Operesheni
hizi zimefanyika siku moja baada ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera
Bunge na Uratibu Jenista Mhagama kutoa taarifa ya Hali ya Dawa za Kulevya
nchini kwa mwaka 2022 ambayo iliitaja mikoa ya Arusha, Iringa, Morogoro na
Manyara kujihusisha na kilimo cha bangi kwa kiasi kikubwa.
Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya kwa kushirikiana na Vyombo vingine vya Ulinzi na Usalama itaendelea kufanya operesheni za mara kwa mara katika maeneo yote nchini ili kuhakikisha kilimo cha bangi na mirungi kinatokomezwa kabisa na wananchi kujikita katika kilimo cha mazao mbadala ya biashara na chakula




Post a Comment