Baadhi ya madiwani wa halmashauri ya wilaya ya Chato wakiwa kwenye kikao cha baraza maalumu la kijadili hoja za CAG.
Mkuu wa mkoa wa Geita,Marthine Shigela,akitoa maelekezo ya serikali kwa watumishi na madiwani wa halmashauri ya wilaya ya Chato
Mkuu wa mkoa wa Geita,Marthine Shigela akizungumza kwenye kikao maalumu cha Baraza la madiwani la kijadili hoja za CAG
***********
Na Daniel Limbe,Chato
SERIKALI mkoani Geita imewapongeza watumishi na madiwani wa halmashauri ya wilaya ya Chato kwa kufanikiwa kupata hati safi ya ukaguzi wa hesabu za serikali kwa kipindi cha miaka mitatu mfululizo.
Pongezi hizo zimetolewa kwa nyakati tofauti na viongozi mbalimbali wa serikali akiwemo mkuu wa mkoa wa Geita,Marthine Shigela,ambaye pamoja na mambo mengine ameonyesha kukerwa na baadhi ya maeneo yaliyoonyesha udhaifu katika utekelezaji wa baadhi ya miradi ya maendeleo.
Kadhalika amewaagiza watumishi wote wa halmashauri hiyo kutimiza wajibu wao kwa lengo la kuhakikisha wilaya hiyo inafikia malengo yanayokusudiwa na serikali.
Alikuwa kwenye kikao maalumu cha Baraza la madiwani kilichoketi leo kwa lengo la kujadili hoja za mkaguzi na mdhibiti mkuu wa hesabu za serikali nchini (CAG) kwa kipindi cha mwaka wa fedha 2021/22.
Hata hivyo,Shigela ametumia fursa hiyo kuwataka madiwani wa halmashauri hiyo kutembelea na kufanya tathimini ya mapato yanayopatikana kwenye vyanzo vya mapato ya ndani vilivyo kwenye kata zao ili kuhakikisha fedha inayopatikana inaakisi uhalisia.
Katibu tawala wa mkoa wa Geita, prof. Godius Kyaharara,amewataka madiwani wa halmashauri hiyo kuwachukulia hatua za kinidhamu baadhi ya watumishi ambao wamekuwa wakisababisha hoja za ukaguzi wa CAG kila mwaka ikiwa ni pamoja na kusimamia maadili ya watumishi wa umma.
Awali mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya hiyo,Christian Manunga,amesema kwa kipindi cha miaka mitatu mfululizo halmashauri yake imeendelea kufanya vizuri kwa kupata hati safi katika ukaguzi wa CAG na kwamba wataendelea kuimalisha mifumo yote ya kiutendaji ili jamii iweze kunufaika na miradi ya maendeleo.
Kwa upande wake,Mkurugenzi wa halmashauri hiyo,Mandia Kihiyo,akaahidi kuufanyia kazi ushauri na maoni yote yaliyotolewa na wadau mbalimbali kwa lengo la kuhakikisha halmashauri hiyo inapiga hatua kubwa za maendeleo.
Mwisho.




Post a Comment