TUTUMIE MFUMO WA KISASA KUKABILIANA NA CHANGAMOTO YA UPUNGUFU WA WALIMU-DC MAPUNDA


..................

Na:Shalua Mpanda -TMC

Wito umetolewa kwa wadau wa elimu nchini kutumia changamoto iliyopo ya upungufu wa walimu kubuni mbinu za kisasa kukabiliana na changamoto hiyo.

Wito huo umetolewa leo  na mkuu wa wilaya ya Temeke mheshimiwa Sixtus Mapunda wakati wa sherehe za mahafali ya kidato cha nne katika shule ya Sekondari Kijichi.

Mhe.Mapunda amesema Serikali inajitahidi kuajiri walimu  lakini haiwezi kumaliza changamoto hii hivyo ni  wakati muafaka sasa kuanza kutumia teknolojia kukabiliana na jambo hili.

"Tumieni walimu wachache waliopo lakini kwa mfumo wa kisasa,Dunia hivi Sasa mwalimu anaweza kuwa darasani lakini akamfundisha mtoto akiwa hapa...kinachotakiwa hapa ni 'internet' na  screen kubwa".Alisema Mkuu huyo wa Wilaya.

Awali akimkaribisha mkuu wa Wilaya,mwalimu mkuu wa Shule hiyo Bi.Catherine Mdachi alisema wamejipanga kufanya vizuri katika mitihani ya kidato cha nne mwaka huu kutokana na juhudi kubwa zinazofanywa na walimu.

Katika hatua nyingine Mhe.Mapunda amewashukuru walimu wanaojitolea katika Shule hiyo ambapo ameahidi kukutana na walimu hao ofisini kwake kuzungumza nao kama motisha kwa kazi wanayofanya.

Serikali ya awamu ya sita chini ya Mhe.Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan imekuwa ikiipa kipaumbele sekta ya elimu kwa kutoa kiasi kikubwa cha fedha katika kuboresha miundombinu ya elimu.


 

0/Post a Comment/Comments