Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Angellah Kairuki ametoa taarifa rasmi Bungeni kuhusu ushindi wa Tanzania wa kuwa mwenyeji wa Mkutano Mkuu wa 50 wa Shirikisho la Wafugaji Nyuki Duniani (50th APIMONDIA Congress).
Taarifa hii imekuja wakati wa kuwasilisha Bajeti ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa mwaka ujao ambapo mkutano huo wa kimataifa utafanyika kuanzia tarehe 20 hadi 25 Septemba, 2027, katika Jiji la Arusha. Mkutano huu utakuwa wa kipekee kwani pia utaadhimisha Jubilee ya Miaka 50 tangu kuanza kwa mikutano ya APIMONDIA. Tukio hili muhimu linatarajiwa kuhudhuriwa na washiriki takribani 6,000 kutoka zaidi ya nchi 130 duniani.
Waziri Kairuki ameainisha faida mbalimbali zinazotarajiwa kutokana na mkutano huu mkubwa, zikiwemo:Kuongeza Teknolojia na Thamani ya Mazao ya Nyuki: Mkutano utaongeza ufahamu na matumizi ya teknolojia mbalimbali za ufugaji nyuki, kuongeza thamani ya mazao ya nyuki na hivyo kuboresha kipato cha wafugaji.
Kuimarisha Mtandao wa Masoko: Kupitia mkutano huu, mtandao wa masoko ya mazao ya nyuki ndani na nje ya nchi utaimarishwa, kuongeza kiwango cha mazao yatakayopelekwa kwenye masoko ya kimataifa.
Kuhamasisha Ufugaji Nyuki Kibiashara: Mkutano utahamasisha ufugaji nyuki kibiashara, jambo ambalo litachangia katika kuongeza ajira, hasa kwa vijana na wanawake.
Kujenga Uwezo kwa Taasisi za Utafiti: Vyuo na taasisi zinazofanya utafiti wa ufugaji nyuki zitapata fursa ya kujenga uwezo zaidi kupitia ushiriki katika mkutano huu.
Kuimarisha Shughuli za Utalii: Shughuli za utalii, hususan utalii wa nyuki (Api-tourism), zitapewa msukumo zaidi kwa kuwashawishi washiriki wa mkutano kutembelea vivutio vya kitalii vilivyopo nchini.

Post a Comment