HALMASHAURI ZATAKIWA KUONGEZA UELEWA KUHUSU UMUHIMU WA TEKNOLOJIA,MKURUGENZI WA HELPAGE TANZANIA ATOA NENO.


 **********

 Na Mwandishi Wetu

Halmashauri na Serikali za Mitaa zimeaaswa kuongeza uelewa kuhusu umuhimu wa teknolojia saidizi kupitia mikutano ya Kijiji, redio za kijamii na vikao vya Halmashauri pamoja na kushirikisha jamii katika kupunguza unyanyapaa kwa watu wenye ulemavu ili kutoa fursa zinazostahili kwa wazee wenye udhaifu na Walemavu badala ya kuwaficha.

 Hayo yamebainishwa Leo Juni 4, 2024 jijini Dar es Salaam na Mkurugenzi Ofisi ya Waziri Kuu, Vijana, Ajira na Watu wenye ulemavu, Rasheed Maftah wakati akizungumza na waandishi wa habari katika kuadhimisha siku ya kimataifa ya teknolojia saidizi Kwa mara ya kwanza nchini Tanzania.

 Amesema kuwa uboreshaji wa teknolojia saidizi ni muhimu Kwa kufanikisha malengo ya maendeleo endelevu (SDGs) na kuhakikisha kuwa hakuna mtu anayeachwa nyuma, ikiwa ni haki muhimu ya binadamu katika kupunguza Umasikini na kutengeneza usawa, hivyo Serikali imechukua hatua kadhaa ikiwa ni pamoja na kuridhia mikakati ya kimataifa kama vile Mkataba wa Mataifa wa Haki za Watu wenye ulemavu, kuandaa sera za Kitaifa za ulemavu ya 2004 na Sera ya Afya ya 2007.

 Kwa upande wake, Mkurugenzi wa HelpAge Tanzania ambao ni wadau katika kuboresha maisha ya wazee nchini, Smart Daniel  amesema wazee wamekuwa wakikabiliwa na changamoto ya kukosa vifaa visaidizi, ambapo karibu asilimia 66 ya wazee wote wanahiyaji aina mojawapo ya vifaa hivyo, na kwa watu wenye ulemavu karibu Milioni 7.1 ya watanzania wote pia Wana mahitaji hayo, hivyo upo umuhimu wa Taifa kuweka mikakati maalum wa upatikanaji wa vifaa visaidizi kwa wenye uhitaji.

Naye Katibu Mkuu wa Shirikisho la vyama vya watu wenye ulemavu Tanzania (SHIVYAWATA), Jonas Lubago ametoa wito Kwa Serikali kuongeza jitihada mbalimbali ikiwemo kuwashawishi wazalishaji wa vifaa visaidizi wa ndani ya nchi ili kupunguza gharama, kuongeza upatikanaji na kufanya vifaa hivyo kuendana na mazingira husika ya Kitanzania.

 Takwimu zinaonyesha kuwa idadi ya watu wanaohitaji Teknolojia Saidizi inaongezeka, huku kidunia ni zaidi ya watu bilioni 2.5, Tanzania ikikadiriwa kuwa na watu Milioni 7.5 wenye uhitaji wa vifaa hivyo, ambapo Kwa mujibu wa Sensa ya watu na makazi ya mwaka 2022, inakadiriwa kuwa  Watu Milioni 3.4 sawa na asilimia 5.7 ya watanzania wote ni wazee, huku ikikadiriwa kuwa ifikapo 2050 idadi ya wazee itafikia Milioni 10.

 

 


0/Post a Comment/Comments