DCEA YAKAMATA KG. 1,815 ZA DAWA ZA KULEVYA AINA YA SKANKA NA WATUHUMIWA WATANO

Kamishna Jenerali wa Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA) wakati akitoa taarifa kwa wanahabari kuhusu operesheni iliyofanyika tarehe 28 Agosti, 2024 hadi tarehe 02 Septemba, 2024 katika maeneo ya Luguruni Mbezi na Magomeni Jijini Dar es Salaam.

Aina ya dawa za kulevya ziulizokamatwa  na  Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA)


..........................

NA MUSSA KHALID

Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA) imekamata  kilogramu 1,815 za dawa za kulevya aina ya skanka pamoja na watuhumiwa watano wanaohusiana na dawa hizo.


Hayo yameelezwa jijini Dar es salaam na Kamishna Jenerali wa Mamlaka hiyo  Aretas Lyimo wakati akitoa taarifa kwa wanahabari kuhusu operesheni iliyofanyika tarehe 28 Agosti, 2024 hadi tarehe 02 Septemba, 2024 katika maeneo ya Luguruni Mbezi na Magomeni Jijini Dar es Salaam


Kamisha Jenerali Lyimo amesema watuhumiwa waliokamatwa wanatambulika kwa majina ya Richard Henry Mwanri (47) ambaye ni mfanyabiashara na mkazi wa Mbezi Makonde wilaya ya Kinondoni jijini Dar es Salaam na Felista Henry Mwanri (70) mkulima na mkazi wa Luguluni Mbezi wilaya ya Ubungo jijini Dar es Salaam ambaye ni mmiliki wa nyumba zilipokutwa dawa hizo za kulevya.


Aidha amewataka watuhumiwa wengine kuwa ni  Athumani Koja Mohamed (58) mfanyabiashara na mkazi wa Tanga, Omary Chande Mohamed (32) dereva bajaji na mkazi wa Buza jijini Dar es Salaam na Juma Abdallah Chapa (36) mkazi wa Kiwalani jijini Dar es Salaam. 


“Richard Mwanri ni mhalifu ambaye amekuwa akipokea dawa za kulevya kutoka nchi mbalimbali na kuziingiza nchini kwa usafiri wa magari zikiwa zimefichwa kwa kuchanganywa na bidhaa nyingine kisha kusambazwa kwa wauzaji wengine katika maeneo mbalimbali nchini” amesema Kamishna Jenerali Lyimo.


Kamishna Jenerali Lyimo amesema katika operesheni hiyo, gari aina ya Mitsubishi Pajero yenye namba za usajili T 551 CAB na bajaji yenye namba za usajili MC 844 CZV vilikamatwa.


Kamishna Jenerali Lyimo amesisitiza kuwa dawa za kulevya ni tishio la usalama kwa jamii na taifa kwa ujumla kwani aina ya skanka inaweza kusababisha kuharibu mifumo ya fahamu na akili magonjwa yasiyoambukiza.


Pia amesisitiza kuwa Matumizi ya skanka kwa wajawazito yanaweza kusababisha madhara kwa mtoto aliye tumboni ikiwemo kuathiri maendeleo ya ubongo na kuzaliwa na uzito mdogo. 


‘Kwa mujibu wa taarifa ya hali ya  Dawa za Kulevya Duniani iliyotolewa Viena nchini Austria tar 26 Juni 2024 iliweka bayana kwamba maeneo yaliyohalalisha matumizi ya Bangi uzalishaji wa bidhaa zenye kiwango kikubwa iliongezeka’ameendelea kusisitiza Kamishna lyimo 


Hata hivyo Mamlaka hiyo imewataka wananchi kuendelea kuonyesha ushirikiano ili hatua mbalimbali ziweze kuchukuliwa kwa watu wanaoharibu maisha ya watu ili kulilinda na kujenga taifa bora la Tanzania.


0/Post a Comment/Comments