******
Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Mhe. Jerry William Silaa (Mb) amesema ujenzi wa kituo cha kuchochea bunifu za TEHAMA (Innovation Hub) kinachotarajiwa kujengwa mkoani Tanga, kitasaidia vijana wa mkoa huo kujikwamua kiuchumi.
Waziri Silaa ameyasema hayo tarehe 23 Januari, 2025 alipotembelea Ofisi za Shirika la Kuhudumia Viwanda Vidogo (SIDO) za Mkoa wa Tanga na kujionea majengo ambayo yakikamilika yatatumika kama kituo cha kuchochea bunifu za TEHAMA (Innovation Hub) mkoani humo.
“Dunia imekuwa kiteknolojia, hivyo vijana wengi kwa ubunifu wao na utundu walioupata shuleni wameweza kubuni teknolojia mbalimbali ambazo zipo mtaani. Hata hivyo, teknolojia hizi zikiwezeshwa, zinaweza kukua. Kuna kampuni nyingi duniani zilizoanzishwa kama startups,” alisema Waziri Silaa.
"Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan anatambua jitihada hizi za vijana wetu na amekuwa akikutana nao. Ametuelekeza wizara kupitia Tume ya TEHAMA kuhakikisha tunawawezesha vijana hawa. Hivyo, tunajenga vituo nane nchi nzima kusaidia vijana hawa," aliongeza Waziri Silaa.
Waziri Silaa alifafanua kuwa vituo hivyo vitajengwa Zanzibar, Dar es Salaam, Mbeya, Arusha, Tanga, Dodoma, Mwanza, na Lindi, na vitawasaidia wabunifu hao kujiendeleza kwa kupata elimu ya namna ya kuendeleza ubunifu wao, kupata maeneo ya kufanyia kazi, na kupata mikopo kutoka taasisi mbalimbali za kifedha.
Akizungumza na waandishi wa Habari baada ya kufika katika eneo hilo, Waziri Silaa alisema kuwa tayari kazi ya kutekeleza mradi huu imeanza kwa hatua mbalimbali ikiwa ni pamoja na kukamilika kwa mikataba minne kati minane ya ujenzi wa vituo hivyo.
“Zikiwa ni jitihada za utekelezaji wa maono ya Rais Samia katika kuwasaidia vijana, nimeelekeza ujengwaji wa kituo hiki uanze haraka,” alisema Waziri Silaa.
Naye, Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Mhe. Balozi Dkt. Batilda Burian, alisisitiza kuwa ofisi yake itasimamia kwa karibu ujenzi wa kituo hicho ili kuhakikisha kinakidhi viwango vilivyowekwa.
Post a Comment