..............................
Na Sophia Malaki
KAMISHNA Msaidizi wa Jeshi la Polisi, Venance Mapala amewataka waumini wa Kanisa Katoliki, Parokia ya Mtakatifu Augustino Ukonga Dar es Salaam kuwaasa watoto wao kutojiingiza kwenye uharifu wa kuharibu miundombinu ya reli ya kisasa (SGR).
Kamishna Mapala ambaye pia ni Afisa wa Polisi jamii Kikosi Cha Reli Tanzania
aliyasema hayo jana kanisani hapo Februari 16 wakati akitoa elimu ya ulinzi wa miundombinu ya reli ya kisasa kwa waumini wa kanisa hilo ambapo alisema ni vema kuondoa dhana kuwa ulinzi wa mali ya reli hiyo ni jukumu la Jeshi la Polisi.
Aliwaasa walezi na wazazi kuwaasa watoto wao kujiepusha na vishawishi vya kuhujumu miundombinu ya reli hiyo ya kisasa ambayo ni mali ya watanzania wote.
"Tuondoe dhana ya ulinzi wa mali ya reli kuwa ni jukumu la jeshi la polisi, serikali au Shirika la Reli Tanzania pekee bali ulinzi wa miundombinu hii ni jukumu letu sote." alisema Kamishina
Mapala na kuongeza kuwa:
"Kila tunapokuja kanisani tunasema tuna muungamania Mwenyezi Mungu, nimekosa mimi, kwa mawazo, kwa vitendo na kwa kutotimiza wajibu, hivyo kutolinda miundombinu ya reli na kusababisha gharama kwa Serikali ni kutotimiza wajibu,
niwasihi tutoe ushirikiano pale panapotokea mtu mwenye nia mbaya kwa ajili ya uharibu ili achukuliwe hatua."alisisitiza.
Aidha Kamishina Mapala alinukuu kifungu katika Katiba ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 ibara ya 27. "ibara ndogo ya kwanza inayosema kila mtu anawajibu wa kulinda mali asilia ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania, mali ya mamlaka ya nchi na inayomilikiwa kwa pamoja na wananchi na pia kuheshimu mali ya mtu mwingine.
Kwa upande wake, Paroko wa kanisa hilo, Padri Martine Dominic alilishukuru Polisi jamii kikosi Cha reli kwa kutoa elimu hiyo kwa waumini na kuendelela kuwakumbusha wananchi kutimiza wajibu wao katika kulinda miundombinu ya reli na maeneo mengine kwa ajili ya maendeleo ya taifa.
Mwisho.
Post a Comment