AIRTEL YAZINDUA KADI YA KIDIJITALI KWA MALIPO YA KIMATAIFA

:::::::

Na Mwandishi Wetu,

Kampuni ya mawasiliano ya Airtel Tanzania, kupitia huduma yake ya Airtel Money, imetangaza uzinduzi rasmi wa huduma ya kadi ya malipo ya kimataifa kwa njia ya kidijitali, ijulikanayo sasa kama Airtel Money Global Pay.

Huduma hiyo mpya imezinduliwa kwa ushirikiano kati ya Airtel Money, Mastercard na kampuni ya teknolojia ya malipo ya kimataifa ya Network International. Kupitia huduma hiyo, wateja wa Airtel sasa wataweza kufanya malipo ya kimataifa moja kwa moja kutoka kwenye simu zao za mkononi, bila kuwa na akaunti ya benki.

Akizungumza wakati wa hafla ya uzinduzi iliyofanyika katika Hoteli ya Johari Rotana jijini Dar es Salaam, Mwenyekiti wa Bodi ya Airtel Money, Adolf Kasegenya, alisema huduma hiyo inaendana na juhudi za Serikali kuhimiza ushiriki wa wananchi katika uchumi wa kidijitali.

“Huduma hii ni sehemu ya kuunga mkono ajenda ya kitaifa ya kukuza uchumi wa kidijitali, ambapo sasa Watanzania wanaweza kufanya manunuzi, kulipia masomo, au huduma nyingine popote duniani kwa usalama na urahisi,” alisema Kasegenya.

Airtel Money Global Pay inapatikana kupitia programu ya MyAirtel App, na inamwezesha mtumiaji kujipatia kadi ya kidijitali papo hapo, kuijaza salio kupitia Airtel Money, na kufanya miamala ya kimataifa kwa kutumia sarafu mbalimbali huku viwango vya ubadilishaji wa fedha vikiwa vinaonekana moja kwa moja.

Kwa mujibu wa Mkurugenzi wa Airtel Money Tanzania, Bw. Andrew Rugamba, huduma hiyo imeboreshwa zaidi ili kutoa suluhisho la uhakika kwa Watanzania wanaofanya manunuzi na shughuli mbalimbali mtandaoni.

“Watumiaji hawahitaji tena akaunti ya benki. Unachohitaji ni kupakua MyAirtel App, kuomba kadi yako ya Global Pay, kuweka salio, na kuanza kutumia huduma hii kulipia bidhaa na huduma kutoka kote duniani,” alisema Rugamba.

Ameongeza kuwa huduma hiyo ni mkombozi kwa Watanzania ambao kwa muda mrefu wamekuwa wakikumbana na changamoto za kufanya malipo ya kimataifa, ikiwemo kadi kutokubalika, ukosefu wa uwazi kwenye viwango vya kubadilisha fedha, na hofu ya usalama wa taarifa za kifedha.

Kwa mujibu wa Airtel, huduma hiyo pia inamwezesha mtumiaji kudhibiti matumizi kwa wakati halisi, kusitisha miamala kwa urahisi, na hata kubadilisha mwonekano wa kadi kupitia simu yake.

Kwa upande wake, Makamu wa Rais wa Mastercard kwa Ukanda wa Telco EEMEA, Kirsten Wottman*, alisema ushirikiano wao na Airtel unalenga kuhakikisha huduma za kifedha salama zinawafikia watu wengi zaidi katika masoko yanayoendelea kama Tanzania.

“Tunataka kuhakikisha kila Mtanzania anapata fursa ya kushiriki kikamilifu katika uchumi wa dunia kupitia miamala salama, hata kama hana akaunti ya benki,” alisema Wottman.

 Uzinduzi wa Airtel Money Global Pay pia umekuja na mabadiliko ya jina kutoka "Airtel Mastercard" hadi jina jipya, huku maboresho zaidi yakijumuisha usalama wa miamala, utumiaji rahisi, na urahisi wa kuunganishwa na huduma nyingine za Airtel Money. 

Huduma hiyo mpya inatarajiwa kusaidia makundi mbalimbali wakiwemo wanafunzi, wafanyabiashara wa mtandaoni, watumiaji wa huduma za burudani, na wasafiri wanaohitaji kufanya malipo ya haraka, salama na kwa gharama nafuu.



 























 ;;;;PICHA ZOTE NA JAMES SAVATORY ;;;;

0/Post a Comment/Comments