WIZARA YA NISHATI YAJIVUNIA UTEKELEZAJI WA MIRADI SABA KATI YA 17 NCHINI

::::::::

Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, Mha. Felchesmi Mramba amesema kuwa katika miradi ya kimkakati inayotekelezwa nchini Wizara ya Nishati inatekeleza takribani miradi saba.

Mhandisi Mramba ameyasema hayo Agosti 17, 2025 wakati wa uzinduzi wa Mpango wa Uwezeshaji wa Kiuchumi kwa Vijana (YEE) ambao unagusa maeneo yanayopitiwa na mradi wa Bomba la Mafuta Ghafi la Afrika Mashariki (EACOP).

“Miradi hiyo ni mradi wa Bomba la Mafuta Ghafi la Afrika Mashariki (EACOP), Bwawa la Julius Nyerere (JNHPP), Mradi wa kugeuza gesi kuwa kimiminika (LNG), Mradi wa utafutaji mafuta, Miradi ya umeme ya Rumakali na Ruhudji na utafiti wa mafuta eneo la Mnazi Bay North”, amesema Mha. Mramba.

Ameeleza kuwa katika miradi hiyo saba, mradi wa bwawa la kufua umeme kwa maji wa Julius Nyerere unaozalisha megawati 2,115 umekamilika na unaingiza umeme kwenye gridi ya Taifa.

Ameongeza kuwa mradi wa bomba la mafuta ghafi (EACOP) umefikia asilimia 65 na upo mbioni kukamilika, mradi wa LNG  upo katika hatua za mwisho na miradi ya umeme ya  Ruhudji na Rumakali tafiti zimekamilika.

Aidha, amesema Serikali ya Tanzania imeshachangia takribani shilingi trilioni 1.12 kwenye mradi wa EACOP kama hisa ya Tanzania katika mradi huo na kuna kampuni za kitanzania 200 ambazo zinatekeleza kazi mbalimbali katika mradi wa EACOP ambazo zitalipwa i jumla ya shilingi trilioni 1.325.

Mhandisi Mramba ametanabaisha kuwa mbali ya fursa za kiuchumi zinazopatikana pia wananchi wa maeneo ambayo  mradi ya umeme inayopeleka umeme EACOP itapita watanufaika kwa kuunganishwa na huduma ya umeme.







 

0/Post a Comment/Comments