WANAJESHI BENIN WATANGAZA KUPINDUA SERIKALI


 ::::::::

Jaribio la mapinduzi linaendelea nchini Benin, baada ya kundi la wanajeshi kudai kwamba wamemwondoa Rais Patrice Talon madarakani na sasa wanachukua usimamizi wa nchi.

Wanajeshi hao, waliounda kile walichokiita “Kamati ya kijeshi”, walionekana kwenye runinga ya taifa Jumapili asubuhi wakitangaza kwamba wamesitisha katiba, kuvunja serikali na kufuta shughuli za vyama vya siasa.

Walijitetea kwa kusema kuwa hatua hiyo imetokana na kutoridhishwa na namna Rais Talon alivyokuwa akiiongoza nchi. Inadaiwa kuwa kundi hilo linaongozwa na Luteni Kanali Pascal Tigri.

Hadi sasa haijafahamika Rais Talon alipo, kwani wanajeshi wameripotiwa kufika katika makazi yake mjini Cotonou. Hata hivyo, shirika la habari la AFP limemnukuu msemaji wa Ikulu likisema kuwa rais yuko salama na jeshi linaanza kurejesha udhibiti.

Milio ya risasi ilisikiwa asubuhi katika mji huo, huku taarifa zikisema helikopta za kijeshi zilikuwa zikizunguka angani juu ya Cotonou.

Ubalozi wa Ufaransa umewataka raia wake kubaki majumbani kwa ajili ya usalama wao.

Benin inatarajiwa kufanya uchaguzi wa urais Aprili 2026, ambao ndiyo mwisho wa muhula wa Rais Talon. Ameshathibitisha kutogombea muhula wa tatu na tayari amemtaja mrithi anayemtaka.

Jaribio hili la mapinduzi nchini Benin limekuja siku chache tu baada ya Rais Umaro Sissoco Embaló kupinduliwa katika nchi jirani ya Guinea-Bissau.

Katika miaka ya karibuni, Afrika Magharibi imekumbwa na misururu ya mapinduzi, hali inayoongeza hofu ya kuzorota kwa usalama wa eneo hilo.

Cc BBC Swahili 

0/Post a Comment/Comments