BALOZI MULAMULA AMLILIA KARDINALI POLYCARP PENGO

::::::::::

Mjumbe Maalum wa Umoja wa Afrika wa Masuala ya Wanawake, Amani na Usalama, Balozi Liberata Mulamula, ametoa salamu za rambi rambi, kufuatia kifo Cha Askofu Mkuu Mstaafu wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam, Kardinali Pengo, kilichotokea usiku wa kuamkia leo.

Balozi Mulamula ametoa salama hizo leo, kutoka nchini Ethiopia ambako anaendelea na majukumu yake mapya ya ujumbe wa wanawake kupitia Umoja wa Mataifa ya Afrika (AU).

"Tutamkumbuka daima Kardinali Pengo kwa unyenyekevu wake na mchango wake mkubwa ambao ulijikita zaidi katika kudumisha amani, kutoa mwongozo wa kimaadili kwa viongozi, na kusemea masuala ya haki za kijamii. Hakusita kukemea maovu kama rushwa na uchochezi wa migogoro ya kidini,"alisema.

Alisema Kadinali Pengo alijulikana kama mtetezi wa amani na mshikamano miongoni mwa Watanzania wa imani zote.

Aliongeza "Askofu Kardinali Pengo, alisisitiza ushirikiano kati ya viongozi wa dini na serikali kuzuia migogoro ya kidini, hususan baada ya mauaji ya viongozi wa dini huko Zanzibar. Itakumbukwa Mwaka 1998 alijitolea kuwa mpatanishi katika mgogoro wa kisiasa visiwani Zanzibar kati ya serikali na chama cha upinzani cha CUF,"alisema.

Balozi Mulamula alieleza kuwa, kwa kutambua mchango wake huo Mwaka 2021, alipewa tuzo ya heshima na Mheshimiwa Rais Dk.Samia Suluhu Hassan kwa mchango wake wa kukuza amani na umoja nchini.

Alisema Kardinali Pengo ataendelea kukumbukwa kwa maisha yake ya Utume uliotukuka na sauti muhimu katika kanisa Tanzania na Afrika kwa ujumla.

"Hakika amevipiga vita vilivyo vizuri, imani ameilinda. Tunamshukuru Mungu kwa zawadi ya maisha yake ya Utume.Pumuzika kwa amani Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo," alisema.

Mwili wa Askofu Kardinali Pengo, utaagwa Februari 27 na kuzikwa Februari 28, Pugu Dar es Salaam.


 

0/Post a Comment/Comments