SULUHISHO LA KUSAMBAZA TAARIFA ZA HALI YA HEWA KWA WAKATI KWA WAKULIMA LAJADILIWA


 ***********

Dar es Salaam, 10 Februari 2026

Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), kwa kushirikiana na Norges Vel na Mpango wa Chakula Duniani (WFP), imekutana na wadau mbalimbali kujadiliana namna ya kufikisha taarifa za hali ya hewa kwa wakati  kwa wakulima.

“TMA itaendelea kushirikiana na wadau wote kuhakikisha taarifa za hali ya hewa na tabianchi zinakuwa rahisi kufikika, kueleweka na kuchochea maamuzi sahihi kwa ajili ya kuimarisha usalama wa chakula na ustahimilivu wa kilimo nchini Tanzania”. Alisema Wilbert Muruke wakati wa ufunguzi wa mkutano kwa niaba ya  Mkurugenzi Mkuu wa TMA .

Alieleza kuwa upatikanaji wa taarifa za hali ya hewa zilizo sahihi na rafiki kwa mtumiaji ni nyenzo muhimu katika kupunguza athari za mabadiliko ya hali ya hewa na tabianchi ili kuongeza tija katika sekta ya kilimo.

Aidha alisisitiza kuwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, imeendelea kuwekeza kwa kiwango kikubwa katika kuimarisha huduma za hali ya hewa, hatua iliyochangia kufikia zaidi ya asilimia 88 ya usahihi wa utabiri wa hali ya hewa nchini. Vilevile, TMA inaendelea kutumia teknolojia za kisasa ikiwemo Akili Unde (AI) na Uchanganuzi wa Takwimu Kubwa (Big Data) ili kuboresha mifumo ya tahadhari za mapema kwa sekta ya kilimo na jamii kwa ujumla.

Kwa upande wake Meneja wa Norges Vel Tanzania Bi,Sesilia Jeremia alisema ‘’mkutano huu ni muhimu kwa kujifunza namna gani mkulima anaweza kupata taarifa za hali ya hewa kwa wakati sahihi ili aweze kufanya maamuzi sahihi kwenye kilimo  haswa zile za siku kumi na teknolojia gani zenye unafuu na endelevu zitumike ili kuleta ufanisi”.

Vilevile kwa upande mwingine mdau wa kilimo na mkulima kutoka Mbarali Bw. Thadeus Mpendakazi alieleza umuhimu wa matumizi ya taarifa za hali ya hewa katika shughuli za kilimo zinasaidia wakulima kupanga aina ya mazao yanaweza kustahimili ukame ama mvua nyingi. 

 Mkutano huo uliwakutanisha wataalamu kutoka TMA, wadau kutoka taasisi za serikali, mashirika ya kimataifa, asasi za kiraia na sekta binafsi kwa lengo la kubadilishana uzoefu, kujifunza na kuimarisha ushirikiano katika kufikisha taarifa za hali ya hewa na tabianchi hadi ngazi ya wakulima wadogo.









0/Post a Comment/Comments