Mamlaka ya Mapato Tanzania kupitia Idara ya Forodha na Ushuru ipo mbioni kuanza kutumia ndege nyuki (Drone) kudhibiti magendo hatua ambayo imetanguliwa na kuanzishwa kwa kitengo cha Drone pamoja na kutolewa kwa mafuzno kwa watumishi watakaofanya kazi katika kitengo hicho.
Akizungumza na waandishi wa habari jijiji Dar es Salaam Februari 13,2026 wakati wa mafunzo ya nadharia ya matumizi ya Drone kwa watumishi wa TRA Idara ya Forodha yanayoendeshwa na Chuo cha Usafiri wa Anga, Naibu Kamishna wa Forodha Utekelezaji na Ufuatiliaji Bw. Felix Tinkasimile amesema hatua hiyo inakuja kuleta mapinduzi katika mapambano dhidi ya magendo.
Amesema Idara ya Forodha na Ushuru inaendelea kuchukua hatua za kimkakati za kuimarisha udhibiti wa magendo na kulinda mapato ya Serikali kwa kutumia teknolojia za kisasa na kuwa kuanza kutolewa kwa mafunzo ya Drone ni sehemu ya mageuzi makubwa ya kuifanya TRA kuwa taasisi ya kisasa inayotumia mifumo bunifu katika usimamizi wa biashara ya kimataifa.
Bw. Tinkasimile amesema kwa muda mrefu, utekelezaji wa operesheni za udhibiti wa magendo ulitegemea kwa kiasi kikubwa taarifa za wasiri pamoja na gharama kubwa za usimamizi wa operesheni za enforcement lakini mfumo wa drone utaleta mabadiliko makubwa kwa kuwezesha ufuatiliaji wa haraka, unaozingatia usalama wa maafisa, kupunguza gharama za doria na operesheni, na kuongeza ufanisi katika kudhibiti vitendo vya magendo.
“TRA imelenga kuwekeza katika drones za kisasa zenye mifumo ya akili mnemba (AI) ambazo zina uwezo wa kuendeshwa umbali mrefu, kuweka kumbukumbu za matukio kwa wakati halisi, na kusaidia uchambuzi wa vihatarishi” amesema Tinkasimile.
Kwa upande wake Mkuu wa mafunzo wa Chuo Cha Usafiri wa Anga Tanzania (CACT) Mweya Didacus amesema zipo faida nyingi za kufahamu namna ya urushaji wa ndege nyuki ikiwemo kurahisisha shughuli mbalimbali na kubaini vitendo vya uhalifu sambamba na kufanya utafiti wa maeneo mbalimbali ambayo wakati mwingine ni vigumu kufikiwa.
Subira Nassoro Mpendekelaki na Saidi Bakari Tindi ni miongoni mwatumishi wanaopatiwa mafunzo hayo ambao wamesema yatawasaidia katika harakati za kupambana na Magendo na kulinda afya za watanzania.







Post a Comment