SERIKALI YAIMARISHA UDHIBITI WA UZITO WA MAGARI, YAONGEZA FURSA KWA WAZAWA

.........

Na Carlos Claudio, Dodoma

Serikali kupitia Wizara ya Ujenzi kwa kushirikiana na Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) imeendelea kuimarisha udhibiti wa uzito wa magari ikiwa ni sehemu ya juhudi za kulinda miundombinu ya barabara na kupunguza gharama za matengenezo zinazotokana na uharibifu wa mapema.

Akizungumza Machi 30, 2026 jijini Dodoma, Kaimu Mtendaji Mkuu wa TANROADS, Efatha Mlavi, alisema kuwa idadi ya mizani isiyohamishika imeongezeka kutoka 67 hadi 79 huku mizani inayohamishika ikiongezeka kutoka 17 hadi 22, hatua inayolenga kuongeza ufanisi wa ukaguzi wa magari barabarani.

Aliongeza kuwa Serikali pia imeweka mizani 20 ya kisasa ya kupima magari yakiwa kwenye mwendo (Weigh-in-Motion) ili kupunguza foleni na kuongeza kasi ya huduma. Aidha, kamera za ulinzi (CCTV) zimefungwa katika vituo 13 vya mizani ili kuimarisha uwazi na uwajibikaji.

Katika hatua nyingine, Mlavi alieleza kuwa tathmini inaonesha ushiriki wa wazawa katika miradi mikubwa bado hauridhishi, ukiwa ni takriban asilimia 10 pekee. Kutokana na hali hiyo, Serikali imeweka mikakati madhubuti ya kuongeza ushiriki huo.

Miongoni mwa mikakati hiyo ni kuhakikisha kazi zote za matengenezo ya barabara na madaraja zinafanywa kwa asilimia 100 na wakandarasi wazawa, ambapo zaidi ya miradi 1,036 yenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 390 hutekelezwa kila mwaka.

Pia, Serikali imetenga asilimia 10 ya bajeti ya maendeleo kwa ajili ya miradi ya mafunzo kwa vitendo, huku miradi minne yenye thamani ya shilingi bilioni 53.6 ikitekelezwa na wakandarasi wanawake wazawa. 

Aidha, angalau asilimia 30 ya bajeti ya maendeleo imetengwa kwa ajili ya kuwapa kipaumbele wazawa na makundi maalum ikiwemo vijana, wanawake na wenye mahitaji maalum.

Katika kuboresha mazingira ya ushindani, Serikali imepanua wigo wa miradi inayotolewa kwa upendeleo kwa wazawa kutoka shilingi bilioni 10 hadi bilioni 50 kupitia maboresho ya sheria ya ununuzi wa umma.

Kuhusu athari za majanga ya asili, Mlavi alisema kuwa kati ya mwaka 2023 na 2024, mvua za El-Nino na Kimbunga Hidaya zilisababisha uharibifu mkubwa wa miundombinu, hali iliyolazimu Serikali kutekeleza miradi 81 ya dharura ya ujenzi wa madaraja katika mikoa 22 kwa gharama ya shilingi bilioni 556.93 kupitia programu ya CERC.

Alisema kati ya miradi hiyo, 70 yenye thamani ya zaidi ya asilimia 74 inatekelezwa na wakandarasi wazawa, na hadi kufikia Machi 2026, miradi 76 imekamilika huku mingine sita ikiwa katika hatua za mwisho katika mikoa mbalimbali ikiwemo Dar es Salaam, Kagera na Ruvuma.

Mbali na ujenzi wa miundombinu, TANROADS pia imeendelea kuwekeza katika kuwajengea uwezo wataalamu wazawa kupitia mafunzo kwa vitendo kwa wanafunzi na wahitimu wa vyuo. 

Mafunzo hayo yanajumuisha usimamizi wa miradi, ujenzi wa madaraja, matumizi ya teknolojia za kisasa pamoja na udhibiti wa ubora wa kazi.

Programu hiyo imetekelezwa katika miradi mikubwa ya kimkakati ikiwemo Daraja la Tanzanite, Daraja la J.P. Magufuli, Daraja la Pangani pamoja na mradi wa bwawa la kuzalisha umeme la Julius Nyerere.

Akizungumzia changamoto, Mlavi alitaja mabadiliko ya tabianchi, ukuaji wa haraka wa miji pamoja na kupanda kwa gharama za vifaa vya ujenzi kuwa ni vikwazo vinavyoathiri utekelezaji wa miradi. 

Alisema TANROADS inaendelea kuchukua hatua mbalimbali ikiwemo ujenzi wa miundombinu imara, upanuzi wa barabara, pamoja na matumizi ya teknolojia mbadala ili kukabiliana na changamoto hizo.

Alitaja pia miradi ya kupunguza msongamano wa magari mijini kama ujenzi wa barabara za mzunguko (Ring Roads), barabara za juu pamoja na mabasi yaendayo haraka (BRT) jijini Dar es Salaam kuwa ni sehemu ya suluhisho la kudumu.

Kwa ujumla, hatua hizi zinaonesha dhamira ya Serikali ya kuimarisha miundombinu ya usafiri, kukuza uchumi wa taifa na kuongeza ushiriki wa wazawa katika miradi ya maendeleo.




 

0/Post a Comment/Comments