*****
Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) imesaini mkataba wa Uboreshaji na Ujenzi wa Miundombinu ya Barabara za Kuelekea na Kuzunguka Uwanja Mpya wa Mashindano ya AFCON-2027 Jiji la Arusha wenye thamani ya Shilingi ya Bilioni 82.9.
Hafla ya utiaji saini imefanyika leo tarehe 20 Machi, 2026 katika uwanja wa AFCON jijini Arusha na kushuhudiwa na mgeni rasmi Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu OWM-TAMISEMI, Mhe. Pro. Riziki Shemdoe (Mb), Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Paul Makonda (Mb), viongozi wa chama na serikali, viongozi wa dini na wananchi wa mkoa wa Arusha.
Akizungumza mara baada ya utiaji saini mkataba huo, Waziri wa Nchi, OWM-TAMISEMI, Mhe. Prof. Riziki Shemdoe amesema fedha za ujenzi wa mradi huo zaidi ya Shilingi Bilioni 80 ni fedha za mapato ya ndani hivyo wananchi wa mkoa wa Arusha wanatakiwa kuitunza miundombinu hiyo.
"Mashindano ya AFCON si mashindano ya Afrika peke yake ni mashindano ya kidunia, barabara hizi za uwanja wa AFCON zinapaswa kuwa bora ndio maana Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ameridhia kutoa fedha kutoka mapato ya ndani kwa ujenzi wa barabara hizi", amesema.
Aidha, Prof. Shemdoe amemtaka Mkandarasi anayetekeleza mradi huo kukamilisha kazi kwa wakati ifikapo mwezi Mei, 2027 kwani hakutakuwa na muda wa nyongeza na amewaomba wananchi wa Arusha wakiona mradi unasuasua wasisite kutoa taarifa sehemu husika ili hatua ziweze kuchukuliwa kwani mradi huo ni kwa faida kwa watanzania.
Mhe. Waziri amemshukuru Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuridhia ongezeko la asilimia 22 kwenye bajeti ya TARURA kwa mwaka wa fedha 2026/27 ili kuboresha mtandao wa barabara za Wakala.
Naye, Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Arusha Mjini, Mhe. Paul Makonda amesisitiza kuwa uwekezaji katika miundombinu ya barabara ni ajenda ya pamoja inayowaunganisha wananchi wote kwani barabara ni kipimo kikuu cha maendeleo ya kijamii na kiuchumi na amewaomba TARURA kusimamia barabara hizo zikamilike kwa wakati.
Awali akitoa taarifa ya mradi huo Mtendaji Mkuu wa TARURA, Mhandisi Victor Seff amesema kuwa barabara zitakazojengwa zina urefu wa kilomita 19.9 kwa kiwango cha lami kuelekea kwenye uwanja kutokea barabara kuu za Arusha–Babati na Arusha Bypass na kuzunguka uwanja.
Amesema barabara hizo ni Mateves-Bondeni kilomita 6.5 (Kilomita 1.5 njia nne na kilomita 5 njia mbili) kutoka barabara kuu ya Arusha–Babati, barabara ya Lendita kilomita 2.75 njia nne, barabara ya Essuri kilomita 2.45 njia nne zote kutoka barabara kuu ya Arusha bypass na kilomita 1.5 barabara kuzunguka uwanja.
Ameongeza kuwa ujenzi wa barabara hizo utajumuisha ujenzi wa Daraja moja (1) la upana wa Mita 100 la zege litajengwa katika barabara ya Essuri, uwekwaji wa taa za barabarani, maeneo ya watembea kwa miguu pamoja alama muhimu za usalama barabarani.
Mkandarasi anayetekeleza mradi huo ni kampuni ya M/s China Railway Construction Engineering Group kwa muda wa miezi 13 akisimamiwa na Mhandisi Mshauri, kampuni ya M/s Afrisa Consulting LTD ya Dar Es Salaam.








.jpg)

Post a Comment