Mwandishi Nguli wa vitabu na mshairi, Bw. Abdilatif Abdalla, ambaye ndiye mgeni rasmi katika halfa ya Tuzo ya Mwalimu Nyerere ya Uandishi Bunifu itakayofanyika kesho, tarehe 13 Aprili 2026, amewasili nchini tayari na kueleza kuwa ni heshima kubwa kwake kupewa hadhi hiyo.
Ameyasema hayo leo, tarehe 12 Aprili 2026, mara baada ya kuwasili katika Uwanja wa Ndege wa kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere akieleza kuwa ni heshima kubwa kwake, kama mwandishi, kutambuliwa na kupewa nafasi ya kuwepo katika tuzo hizo.
“Hii ni heshima kubwa kwangu kama mwandishi kupata hadhi hii ya kuwa mgeni rasmi katika tuzo zenye kutambua kazi ya Hayati Nyerere ya kukuza Kiswahili duniani kote”amesema Prof.Abdalla.
Kwa upande wake , Mwenyekiti wa kamati ya Tuzo, Prof. Penina Mlama ameonesha kufurahishwa na ujio wa mgeni rasmi na kueleza kuwa, kwa waandishi bunifu nchini ni fahari kuwa na mgeni rasmi ambaye pia ni mwandishi mwenzao.
Naye Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Elimu Tanzania (TET), taasisi ambayo ndiyo mratibu wa Tuzo hiyo amewakaribisha wageni wote katika hafla hiyo inayolenga kuendeleza uandishi bunifu na kuhamasisha utamaduni wa usomaji wa vitabu nchini.
Tuzo hizo hufanyika kila mwaka tarehe 13 Aprili kwa lengo la kuadhimisha kumbukumbu ya kuzaliwa kwa Baba wa Taifa, Hayati Julius Kambarage Nyerere.








Post a Comment