THTU YATAKA UTAFITI UBADILISHWE KUWA MAPATO NA AJIRA

 

Na Mwandishi Wetu, DODOMA

Chama cha Wafanyakazi wa Taasisi za Elimu ya Juu Tanzania (THTU) kimeitaka Serikali kuweka mfumo madhubuti wa kubadilisha tafiti na ubunifu kuwa bidhaa, huduma na ajira ili kuchochea ukuaji wa uchumi wa taifa.

Hayo yamo katika andiko la utafiti na mapato lililowasilishwa serikalini, likilenga kuunganisha utafiti wa kitaaluma na mahitaji ya soko chini ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari na Mwenyekiti wa THTU Taifa, Dk. Paul Loisulie, licha ya Tanzania kuwa na wingi wa tafiti na ubunifu, matokeo yake hayajatumika ipasavyo kuleta maendeleo ya kiuchumi.

Alisema tafiti nyingi hubaki katika ngazi ya kitaaluma bila kubadilishwa kuwa bidhaa au huduma, hali inayopunguza mchango wake katika uchumi.

“Tunahitaji mfumo wa kitaifa unaounganisha utafiti, ubunifu na biashara ili kufungua fursa za ajira na mapato,” alisema.

THTU imependekeza kuanzishwa kwa mifumo ya ufadhili wa ubunifu, kuimarisha ushirikiano kati ya vyuo vikuu na sekta binafsi, pamoja na kuongeza uwekezaji katika utafiti na maendeleo.

Aidha, chama hicho kimebainisha kuwa kuwekeza katika ubunifu na teknolojia kutasaidia Tanzania kujenga uchumi wa maarifa na kuongeza ushindani katika soko la kimataifa.

Kwa mujibu wa THTU, hatua hiyo ni muhimu katika kuhakikisha tafiti zinazozalishwa nchini zinakuwa na manufaa ya moja kwa moja kwa jamii na taifa kwa ujumla.

0/Post a Comment/Comments