****
Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Bw. Yusuph Juma Mwenda, amesema ni heshima kubwa kwa Tanzania kuwa mwenyeji wa Mkutano wa Shirika la Forodha Duniani Kanda ya Mashariki na Kusini mwa Afrika (WCO ESA Regional Meetings) unaowakutanisha wataalamu wa forodha kutoka mataifa 24 na kujadili namna ya kuimarisha usalama wa mipaka, biashara na ukusanyaji wa mapato ya Serikali.
Akizungumza akiwa Mgeni Rasmi wakati wa mkutano huo uliofanyika Jumatatu Mei 11, 2026 katika Ukumbi wa Hoteli ya Golden Tulip nje kidogo ya mji wa Zanzibar, Bw. Mwenda amesema Idara za forodha zina jukumu kubwa la kulinda mipaka ya nchi kwa kuzuia uingizwaji wa bidhaa zisizoruhusiwa kuingia nchini ikiwemo madawa ya kulevya, uingizaji wa silaha kinyume na sheria, magendo huku akieleza kuwa ushirikiano baina ya nchi ni muhimu katika kukabiliana na vihatarishi hivyo bila kuathiri biashara halali.
Aidha, amesema mkutano huo umejikita katika kujadili namna ya kurahisisha biashara kwa kutumia mifumo ya kisasa ya forodha ili kuhakikisha wafanyabiashara hawacheleweshwi wanapofanya shughuli zao.
Bw. Mwenda, ameeleza kuwa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kupitia mfumo wa TANCIS imeendelea kurahisisha michakato ya forodha na kuongeza uwazi katika utoaji wa huduma kwa wateja.
Pamoja na hayo, amesema nchi nyingi bado zinakabiliwa na changamoto za ukwepaji kodi ikiwemo udanganyifu wa thamani ya bidhaa, rushwa pamoja na vitendo vya maafisa wasio waadilifu, hali inayopunguza mapato ya Serikali na kuathiri ushindani wa biashara.
Kutokana na hilo, mesisitiza umuhimu wa kuchukua hatua za kudhibiti vihatarishi hivyo kupitia mifumo madhubuti ya usimamizi na matumizi ya teknolojia za kisasa.
Katika hatua nyingine, amesema nchi wanachama wa WCO ESA, zinatakiwa kuendelea kuwekeza katika mifumo ya kisasa ya forodha, vifaa vya kudhibiti magendo pamoja na kubadilishana taarifa baina ya nchi ili mifumo ya forodha iweze kusomana na kuongeza ufanisi wa utekelezaji wa sheria.
Mbali na hayo, ametoa wito kwa wananchi na wafanyabiashara kuendelea kushirikiana na TRA kwa kutoa taarifa kuhusu wafanyabiashara wasio waaminifu wanaojihusisha na magendo na ukwepaji kodi huku akisisitiza kuwa Serikali imeendelea kuboresha mazingira ya biashara kwa kupunguza baadhi ya kodi na kuweka utaratibu wa wazi unaorahisisha utoaji wa mizigo katika maeneo ya forodha ili kuwahudumia walipakodi kwa ufanisi zaidi.

Post a Comment