NA: MWANDISHI WETU, GEITA
Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) na Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM Taifa (MCC), Mary Chatanda amepongeza ziara ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan aliyoifanya nchini Urusi Juni 3 hadi 5, 2026, kuwa ina tija kubwa katika kukuza maendeleo ya nchi.
Chatanda ameyasema hayo Juni 7, 2026, mkoani Geita, kufuatia kumalizika kwa ziara hiyo. Chatanda amesema Tanzania si kisiwa, tunapaswa kushirikiana na mataifa mengine hasa katika kuitangaza fursa za kijamii na kiuchumi zilizopo nchini ili tushirikiane nao katika kukuza maendeleo.
"Tanzania hatupaswi kujifungia, inabidi tutoke kusaka fursa katika sekta mbalimbali kama kilimo, biashara, nishati, madini, utalii, afya, maji, umeme na elimu. Rais Dk. Samia ametangaza fursa mbalimbali zilizopo na tayari wenzetu wa Urusi wameonyesha utayari wao wa kushirikiana na sisi," amesema Chatanda.
Sambamba na hilo, Chatanda amesisitiza kuwa Rais anaposafiri kwenda nje ya nchi ni kwa ajili ya kukuza diplomasia ya uchumi, ambapo matunda yake ni makubwa katika kukuza maendeleo endelevu.
Ikumbukwe kuwa Rais Dk. Samia alifanya ziara nchini humo ikiwa ni juhudi za kukuza maendeleo. Juni 5, Rais Dk. Samia alipata wasaa wa kuhutubia Jukwaa la Kimataifa la Uchumi la St. Petersburg (SPIEF 2026).
Katika hotuba yake, Rais Dk. Samia alinadi fursa mbalimbali zinazopatikana nchini Tanzania zikiwemo madini, kilimo, nishati safi, utalii, afya na dawa.
Fursa nyingine ni usafirishaji, ugavi, biashara, mafuta na gesi huku wafanyabiashara na wawekezaji wa Urusi wakialikwa kuwekeza Tanzania. Ziara hiyo inatokana na mwaliko wa Rais Vladimir Putin wa Urusi.






Post a Comment