WAZIRI MKUU AMSIFU KAFULILA, ASEMA NI KIONGOZI KIJANA MWENYE UPEO MPANA

*****

Amtaja Kama Kiongozi Kijana Mwenye Exposure ya Kimataifa

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mwigulu Nchemba, amemsifu Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (PPP Centre), David Kafulila, akimtaja kuwa ni miongoni mwa viongozi vijana wenye uwezo wa kuelewa mwenendo wa maendeleo duniani na kutumia uzoefu huo kusukuma mageuzi nchini.

Akizungumza leo Jumanne, Juni 30, 2026, wakati wa Uzinduzi wa Mfumo wa Tanzania Chamber Portal na Mkutano wa Mwaka wa Biashara na Uwekezaji 2026, Waziri Mkuu amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuwaamini vijana katika nafasi za uongozi kutokana na uwezo wao wa kuleta matokeo.

Amemtaja Kafulila kama mfano wa viongozi hao, akisema ana upeo mpana wa masuala ya maendeleo na hufuatilia mifumo iliyofanikiwa katika nchi mbalimbali ili kuitafsiri katika mazingira ya Tanzania.

"Kwa bahati nzuri sana Rais Samia ameamini vijana katika kila eneo. Ukienda PPP Centre yuko ndugu yangu Kafulila, ni kijana tena mwenye exposure (upeo mpana) , ni msomi wa current affairs (masuala ya sasa ya kitaifa na kimataifa) maana ni mmoja wa vijana wanaoelewa waliofanikiwa wamefanikiwaje katika nchi mbalimbali," alisema Waziri Mkuu.

Katika hotuba yake, Waziri Mkuu amesisitiza kuwa ajenda ya sekta binafsi sasa ni ajenda ya Taifa, akieleza kuwa utekelezaji wa Dira ya Taifa 2050 unategemea kwa asilimia 70 mchango wa sekta binafsi, hivyo ushirikiano kati ya Serikali na wafanyabiashara unapaswa kupewa kipaumbele.

Aidha, alisema Rais Dkt. Samia ametoa ridhaa ya kuondoa vikwazo vya kisheria vinavyokwamisha biashara na uwekezaji, akisisitiza kuwa endapo kuna sheria zinazozuia maendeleo zipelekwe bungeni zifanyiwe marekebisho ili kuharakisha utekelezaji wa ajenda ya maendeleo ya Taifa.




0/Post a Comment/Comments