TEA YAWAOMBA WADAU KUCHANGIA MFUKO WA TAIFA WA ELIMU KUIMARISHA ELIMU YA AMALI

..........

Na Carlos Claudio, Dar es Salaam

Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA) imezitaka taasisi za maendeleo, sekta binafsi na Watanzania kwa ujumla kujitokeza kuchangia Mfuko wa Taifa wa Elimu ili kuongeza rasilimali zitakazowezesha uwekezaji mkubwa katika elimu ya amali na kuwajengea vijana ujuzi wa kujiajiri na kuchochea ukuaji wa uchumi wa taifa.

Wito huo umetolewa leo Julai 11, 2026 na Mjumbe wa Bodi ya Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA), Godfrey Boniventura, alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari katika banda la TEA kwenye Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara (Sabasaba), yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere, jijini Dar es Salaam.

Boniventura amesema TEA imeanzishwa kisheria kusimamia Mfuko wa Taifa wa Elimu kwa jukumu la kutafuta na kuratibu rasilimali zinazolenga kuboresha sekta ya elimu nchini, hususan ujenzi na uboreshaji wa miundombinu pamoja na kuimarisha utoaji wa elimu yenye kuendana na mahitaji ya sasa.

Amesema utoaji wa elimu si jukumu la Serikali pekee, bali ni wajibu wa wadau wote wa maendeleo, sekta binafsi na wananchi kushiriki katika kuchangia Mfuko wa Taifa wa Elimu ili kuhakikisha sekta hiyo inapata fedha za kutosha kwa ajili ya kuwekeza katika maendeleo ya elimu.

"Rai yetu kubwa kama Bodi, kwa kushirikiana na menejimenti ya TEA, ni kuwaomba wadau wa maendeleo, sekta binafsi na Watanzania wote wenye uwezo kujitokeza kuchangia Mfuko wa Taifa wa Elimu. Fedha hizo zitasaidia kuongeza uwekezaji katika elimu inayowajengea watoto wa Kitanzania ujuzi wa kujitegemea," amesema.

Ameeleza kuwa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inaweka mkazo mkubwa katika maendeleo ya ujuzi, hivyo ni muhimu mfumo wa elimu uzalishe wahitimu wenye maarifa na stadi zinazowawezesha kujiajiri na kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya uchumi.

Boniventura amesema sera ya elimu ya sasa imeweka msisitizo katika maeneo mawili makuu ambayo ni elimu ya jumla na elimu ya amali, huku TEA ikielekeza nguvu zaidi katika kuhamasisha uwekezaji kwenye elimu ya amali ili kuhakikisha wanafunzi wanahitimu wakiwa na ujuzi unaokidhi mahitaji ya soko la ajira.

Amesisitiza kuwa TEA itaendelea kushirikiana na Bodi yake kuhakikisha inatafuta rasilimali nyingi zaidi na kuzielekeza katika miradi inayokuza elimu ya amali, hatua ambayo itasaidia kuzalisha kizazi cha vijana wenye ujuzi na uwezo wa kuchangia maendeleo ya taifa.

Aidha, ametoa shukrani kwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Wizara ya Elimu kwa kuendelea kuipa TEA ushirikiano mkubwa katika kutekeleza majukumu yake, huku akiitaka Serikali kuendelea kuwahamasisha wadau mbalimbali kutambua kuwa kuboresha elimu ni jukumu la kila Mtanzania na si Serikali pekee.

"Ninaamini tukishirikiana wote katika kuchangia Mfuko wa Taifa wa Elimu, tutaiwezesha Tanzania kuwa na mfumo wa elimu unaozalisha vijana wenye ujuzi, wabunifu na wanaoweza kujitegemea," amesema Boniventura.


 

0/Post a Comment/Comments