Na Mwandishi Wetu, Dodoma
DODOMA: Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Hamad Chande, ameziagiza taasisi zote zilizo chini ya wizara hiyo, ikiwemo Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), kuongeza matumizi ya mitandao ya kijamii na teknolojia za mawasiliano kutangaza bidhaa, huduma na vivutio vya sekta ya maliasili, akisema hatua hiyo itapanua masoko, kuvutia watalii na kuongeza mchango wa sekta hiyo katika uchumi wa Taifa.
Akizungumza baada ya kutembelea Banda la Wizara ya Maliasili na Utalii katika Maonesho ya Nanenane yanayoendelea Viwanja vya Dkt. John Malecela, Nzuguni, Dodoma, Agosti 6, 2026, Chande alisema dunia imehamia katika majukwaa ya kidijitali, hivyo taasisi zinapaswa kutumia fursa hiyo kuwafikia wananchi na masoko mapya ndani na nje ya nchi.
“Ulimwengu leo umehama kutoka kwenye vitabu na maandishi ya kawaida kwenda kwenye mitandao. Tuyaonyeshe maonesho yetu kwenye mitandao na tuongeze nguvu katika majukwaa yote ya kijamii ili watu wengi zaidi wajifunze na kuzifahamu fursa zilizopo,” alisema Mhe. Chande.
Alisema sekta ya maliasili ina hazina kubwa ya fursa za kiuchumi kupitia utalii, mazao ya misitu, bidhaa za nyuki na huduma za uhifadhi, lakini manufaa yake yataongezeka zaidi endapo bidhaa na huduma hizo zitatangazwa kwa ubunifu na kufikishwa katika masoko mapana.
Naibu Waziri huyo pia alisisitiza kuwa elimu ya uhifadhi wa misitu na wanyamapori inapaswa kuendelea kutolewa kwa wananchi kwa kuwa uhifadhi ndio msingi wa maendeleo endelevu na ukuaji wa sekta nyingine muhimu za uchumi, ikiwemo kilimo.
Akizungumzia kaulimbiu ya Nanenane mwaka huu ya “Tambua Soko; Ongeza Tija Kutekeleza Dira 2050,” Mhe. Chande alisema taasisi zote zinapaswa kuitafsiri kwa vitendo kwa kuboresha uzalishaji, kuongeza ubora wa bidhaa na kuzitafutia masoko mapya ili kuinua kipato cha wananchi na kukuza uchumi wa Taifa.
Aidha, alimpongeza TFS kwa elimu ya vitendo inayotolewa katika banda lake, akisema inawasaidia wananchi kufahamu fursa zilizopo katika sekta ya misitu, ufugaji nyuki na uhifadhi pamoja na namna ya kuzitumia kujiongezea kipato.
Pia aliwataka wananchi wanaojishughulisha na biashara ya mazao ya misitu kufuata sheria, kanuni na taratibu zilizowekwa ili kuepuka usumbufu usio wa lazima na kuhakikisha rasilimali za misitu zinatumika kwa njia endelevu huku zikichangia ukuaji wa uchumi.





Post a Comment