**********
Chama cha Wafanyakazi Wakusanya Mapato Tanzania (TAREWU) kimesaini Hati
ya Makubaliano (MoU) na TIB Rasilimali Limited, kwa lengo la kuimarisha elimu
ya fedha na ustawi wa kiuchumi wa wanachama wake.
Hati hiyo imesainiwa leo, Septemba 14, 2026, katika ofisi za TIB
Rasilimali Limited, Mlimani City, Dar es Salaam, ambapo ushirikiano huo
unalenga kuwajengea wanachama uwezo wa kusimamia mapato na matumizi, kuweka
akiba, kupanga fedha na kufanya uwekezaji wenye tija.
Akizungumza katika hafla hiyo, Katibu Mkuu wa TAREWU, Dkt. Michael Marere, amesema ustawi wa mwanachama hauishii kwenye masuala ya maslahi ya kikazi pekee, bali unahusisha pia uwezo wa kusimamia kipato na kufanya maamuzi sahihi ya kifedha.
Katibu Mkuu wa TAREWU, Dkt. Michael Marere,akizungumza katika hafla ya utiliaji Makubaliano (MoU) na TIB Rasilimali Limited, kwa lengo la kuimarisha elimu ya fedha na ustawi wa kiuchumi wa wanachama wake.Amesema TAREWU imeweka elimu ya fedha na ustawi wa kiuchumi kuwa
miongoni mwa vipaumbele katika Mpango Mkakati wake wa Pili wa mwaka 2026–2030,
hivyo ushirikiano huo ni hatua muhimu katika kutekeleza azma hiyo kwa vitendo.
Dkt. Marere amesema TAREWU inalenga kujenga “mwanachama mwenye maarifa,
mwenye uwezo wa kifedha na mwenye ustawi,” huku akisisitiza kuwa elimu ya fedha
inapaswa kuwa utamaduni endelevu na si tukio la mara moja.
Amesema kupitia ushirikiano huo, wanachama watawezeshwa kuelewa na kupanga matumizi ya fedha, kujenga akiba, kuwekeza kwa uelewa na kufanya maamuzi yatakayosaidia kulinda ustawi wao na familia zao kwa sasa na baadaye.
Mkurugenzi Mtendaji wa TIB Rasilimali Limited, Brighton Kinemo, akizungumza katika hafla ya utiliaji Makubaliano (MoU) na TAREWU , kwa lengo la kuimarisha elimu ya fedha na ustawi wa kiuchumi wa wanachama wake.Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa TIB Rasilimali Limited, Brighton
Kinemo, amesema utekelezaji wa makubaliano hayo utawawezesha wafanyakazi wa
TAREWU kupata elimu ya fedha na uwekezaji itakayowasaidia kujimarisha kiuchumi
kabla na baada ya kustaafu.
Kinemo amesema elimu ya fedha ni muhimu kwa mfanyakazi, akisisitiza kuwa
kufanya kazi kwa miaka mingi pekee hakutoshi bila kuwa na uelewa wa namna ya
kusimamia fedha na kuwekeza. “Mtu anaweza kufanya kazi kwa miaka mingi lakini
suala la msingi ni, una elimu gani ya fedha na uwekezaji?” amesema.










Post a Comment